FAHAMU KILIMO CHA KARANGA KINAVYOBORESHA MAISHA YA WAKAZI WA BUKOMBE


 Vijana wakazi wa kata ya Lyambamgongo wilaya ya Bukombe wakimenya karanga tayari kwenda sokoni

"Na watoto kwa umoja, wakakumbuka kauli, Kama mnataka mali, mtayapata shambani"

 Ni kati ya mistari ya kuvutia kwenye shairi la 'Karudi baba mmoja' ambalo waliosoma shule za umma nchini Tanzania enzi hizo wanalihusudu kutokana na utajiri unaopatikana kwenye kilimo.

Aidha, shairi hilo hushamirishwa na methali ya Kiswahili isemayo  "Jembe halimtupi mkulima." Ikiwa na maana kwamba mtu yeyote anayeshika jembe na kwenda shambani kulima lazima atapata chochote kitu.

Wapo ambao kwao mashairi na methali hazikubaki hadithi tamu za shule bali darasa la mafanikio kama ilivyo kwa Pius Vasco kutoka kata ya Lyambamgongo wilaya ya Bukombe, Geita.

 

Katika Makala haya, tunamwangazia mkulima Pius Vasco. Ambatana nasi!

Pius Vasco akiwa katika moja ya mashamba yake ya karanga

 Bukombe Sasa ilipofika nyumbani kwa Pius ilikuwa majira ya saa 6:00 mchana siku ya Alhamisi Novemba 16, 2023 ambapo ilipokelewa na mkewe Vicky Manyabuluba pamoja na watoto waliokuwa wakisaga karanga kwa ajili ya maandalizi ya mlo wa mchana.

Kabla ya kujitambulisha kwanza nilishangazwa na kiwango cha utajiri nilichokiona pale ikiwemo nyumba ya  kisasa yenye umeme, mifumo ya mawasiliano, maji na sura zenye afya na hivyo kuuliza.. "hapa ni kwa Pius Vasco?" Nikujibiwa "Ndiyo" Nikauliza tena "anafanyakazi gani?" Nikajibiwa " hana kazi, yupo tu. Nimkulima"

Hata hivyo,Vicky alinihakikishia kuwa Pius Vasco asingechelewa kufika nyumbani kwani alikuwa tayari amempigia simu kumjulisha ujio wangu na Pius anamiliki usafiri (chombo cha moto) pikipiki na mashamba yake hayapo umbali mrefu hivyo nivute subira.

Wakati namsubiri Pius huku Vicky akiendelea kusaga karanga, kichwani kauli ya "hana kazi, ni mkulima tu" inanisumbua. Jakaya Kikwete naye ni mkulima mzuri tu, Mizengo Pinda, Mjwahuzi Karushaija, Masanja Mkandamizaji "lakini hawa uenda walipata mitaji mikubwa. Lakini Jesse Robert mbona alianza bila mtaji wowote zaidi ya ardhi na jembe?"

Ghafla kijana wa miaka 41 baba wa watoto saba aliyehitimu darasa la saba 1998, mpole mwenye rangi ya maji ya kunde, Pius Vasco anafika ambapo namuuliza kama anafahamu kuwa Novemba kila mwaka huadhimishwa kama  mwezi wa karanga duniani?


Mkulima wa karanga Pius Vasco kutoka kata ya Lyambamgongo wilaya ya Bukombe Geita akiwa amepumzika nyumnai kwake na familia baada ya kutoka shambani huku mkewe Vicky akisaga karaga kwa lengo la kuandaa mboga ya chakula cha mchana kwa familia hiyo


Pius anakiri kuwa alianza kulima karanga kisasa kwa mbegu bora katika kipindi cha Mbunge Doto Biteko na utawala wa Said Nkumba wilayani humo baada ya wataalamu kufika kijijini hapo na kuanza kupokea mbegu bora kutoka kituo cha Naliendele.

Aidha, alieleza kupatiwa msaada wa malezi shambani na Afisa Kilimo wa kata ya Lyambamgongo, Lydia Mtindo na hata kuweza kuunda kikundi cha wakulima 10 ambapo kati yao wanawake ni wane. Lengo la kikundi hicho ni kuwezesha kufikiwa kirahisi na wataalamu pamoja na kutoa hamasa kwa wanakijiji wengine kuweza kulima kisasa.

Anataja faida za kikundi hicho kuwa ni pamoja na kusaidiana wakati wa kupanda, kukumbushana wakati sahihi wa kupanda na kuvutia mitaji.

 

 

Baadhi ya wakulima wa Lyambamgongo wakiwajibika katika shamba la karanga

"Usione tunapata faida, kuna kazi kubwa kwenye kupanda. Kutoka shimo moja hadi lingine unatakiwa uache sentimita 10 na mstari hadi mstari ni sentimita 50. Hivyo utaona ilivyokazi kupanda ekari moja na zaidi peke yako." alisema Pius

Aliongeza kuwa baada ya kuacha kilimo cha mazoea na kuanza kulima kufuata ushauri wa wataalam kumekuwa na ongezeko la mavuno na kipato jambo lililomwezesha kujenga nyumba zaidi ya moja, kununua pikipiki na kukidhi mahitaji ya familia ikiwemo lishe, matibabu na shule.

“Baada ya kupatiwa mafunzo na mbegu bora kutoka Naliendele, eneo ambalo awali niliweza kuvuna gunia 15 sasa hivi navuna hadi gunia 30 eneo hilohilo” alifafanua

 

Gunia moja la karanga huuzwa kati ya shilingi 65,000 hadi 100,000 kutegemea na msimu. Alisema wateja wao wakubwa ni kutoka nchi za Burundi, Rwanda, Uganda na wenyeji wa Tanzania kutoka mikoa ya Mwanza na Shinyanga ukiacha soko la ndani ya wilaya ambao ununua kwa matumizi ya chakula.

Mwanakikundi, Edson Hamphrey alilieza Bukombe Sasa kuwa mbali na kuuza karanga ghafi, amekuwa akijipatia pia mafuta ya kupikia kutokana na zao hilo.

“Huwa namenya naziosha, nasaga, nakamua mafuta. Katika gunia moja Napata hadi lita 25 za mafuta. Mafuta ya karanga ni bora kuliko mafuta mengine” alisimua Hamphrey

 

Hamphrey ambaye awali aliishi eneo la Pasians Jijiji Mwanza akijishughulisha na biashara ndogondogo (umachinga) baada ya kutoka nyumbani kwao Singida kutafuta maisha, anasema aliamua kwenda wilayani Bukombe baada ya kuelezwa na marafiki zake juu ya fursa zilizomo katika wilaya hiyo ikiwa ni baada ya utawala Mashishanga kuzuia biashara holela mkoani Mwanza.

Kwa upande wake Elizabeth Hosea ambaye pia Mwenyekiti wa mtaa wa Lyambamgongo alisema kuwa aliamua kujiunga na kikundi kutokana na faida anazoziona kwa wengine wanaolima kwa kufuata ushauri wa wataalam.

 

“Kilimo kimeniwezesha kusomesha watoto na pia kuanzisha ujasiliamali mwingine mdogo mdogo kama unavyoona pale (anaonesha grocery yake) na pia nafuga na kuku” alieleza faida Elizabeth akiwa kwenye shamba lake karibu na barabara kuu ya Rusumo-Kahama aliloliita shamba darasa.

Mwalimu Moses Nyahiti ambaye amejiingiza kwenye kilimo baada ya kustaafu utumishi wa umma, alisema kuwa kilimo kimemuwezesha kuendelea kuishi kama ambavyo ilikuwa wakati akiwa kazini.

“Kwenye kilimo napata kipato kizuri hususani kwenye karanga. Nyie mnaita maokoto? Kwenye kilimo maokoto yapo” alieza Mwalimu Nyahiti huku akitabasamu

Aprili 2023, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Said Nkuba alijitolea kuhamasisha ulimaji wa karanga katika wilaya hiyo baada ya yeye mwenyewe kulima na kuona faida yake kiuchumi.

Nkumba alitoa ahadi hiyo alipotembelewa na watafiti wa Zao la Karanga kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania TARI kituo cha Naliendele ambao walifika wilani humo kuona majaribio ya mbegu ya zao hilo.

Alisema kuwa wilaya hiyo ina ardhi nzuri yenye rutuba hivyo inafaa kwa kilimo cha karanga kwakuwa karanga hazihitaji mbolea wala viwatilifu na kuagiza wakulima kupatiwa elimu ili waweza kuzalisha zaidi.

“Niko tayari kufanya uhamasisha wa zao la karanga katika wilaya yangu ili kuwezezsha wakulima kulima kwa wingi zaidi"

“Nitawaunga mkono pale mtakapo hitaji uwepo wangu kwakuwa mimi ni mkulima mzuri wa zao hili. Napata pesa nyingi kwa kulima karanga.  Wakulima wanaweza kubadili hali zao kupitia karanga ” alisema Nkumba


Mkuu wa wilaya Bukombe, Said Nkumba akiwa shambani wilayani humo ikiwa ni moja ya hamasa kwa wakulima Novemba, 2023

Kwa upande wake Afisa Kilimo kata ya Lyambamgongo, Lydia Mitindo alisema kuwa kumekuwa na mwitikio mkubwa kwa wakulima wa kata hiyo kulima kisasa baada ya kuona faida ambazo wengine wanapata kutokana na kilimo hicho.

“Tumeamua kuanzisha kikundi ili kukitumia kama darasa pamoja na kuwavuta wenzao japo changamoto ni watu kukubali kubadilika kwa haraka" alisema Lydia.

 

Afisa Kilimo kata ya Lyambamgongo, Lydia Mitindo akiwa shambani tayari kutoa ushauri kwa wakulima wa kata hiyo

Mbali na faida za kibiashara, karanga hutoa mchango mkubwa katika kuboresha afya ya binadamu.

Kwa mujibu wa taasisi ya chakula na dawa ya Marekani USDA, karanga ina utajiri wa protini, mafuta mazuri, nishati, nyuzi lishe, madini chuma, calcium, magnesium, potassium, zinc na phosphorus

Pia inaelezwa kuwa karanga huwa na kampaundi za resveratrol ambazo huongeza ubora wa afya ya uzazi kwa wanaume pamoja na uwezo wa kuongeza kiasi cha mafuta mazuri mwilini ambayo huwa na faida kwenye afya ya moyo.

Novemba kila mwaka huadhimishwa kama mwezi wa Wapenda karanga duniani. Watu wengi dunia huita mwezi huu kuwa mwezi wa Wazimu wa Siagi ya Karanga!

Historia ya Mwezi wa Siagi ya Karanga huambana na historia nzima ya siagi yenyewe na kuenea kwa karanga duniani.

Karanga ni jamii ya kunde ambayo asili yake ni Amerika Kusini, na imekuwepo duniani kwa takribani miaka 7600.

Ingawa asili ya kitu kama siagi ya karanga inaweza kufuatiliwa hadi kwa Waazteki na Wainka, historia

yake ya kisasa inaonekana ilianza mnamo 1884, wakati ilipewa hati miliki na Mkemia wa Kimarekani anayejulikana kwa jina la Edson.

Madhumuni yake yote ya kuikuza ilikuwa ni kuhakikisha kwamba wale ambao walikuwa na matatizo ya kutafuna vyakula vigumu wangeweza kuwa  na njia ya ladha ya kupata lishe waliyohitaji. Hivyo, siagi ya karanga ilizaliwa.

Tangu wakati huo, tiba hii ya ladha na lishe imelipuka hadi kwenye eneo la upishi katika kila ruhusa inayowezekana na inaweza kupatikana kwa tofauti fulani katika aina fulani katika milo tofauti tofauti.

Mnamo 1995, Mwezi wa Wapenda Siagi ya Karanga ulianza na umekuwa ukiadhimishwa tangu wakati huo katika tamasha la mwezi mzima la siagi ya karanga!

Jinsi ya kuadhimisha Mwezi wa Wapenda Siagi ya Karanga ili kwenda sawa na Mwezi wa Wapenda Siagi ya Karanga.

Fanya hivi!


Vicky akisaga karanga kwa ajili ya mboga ya mchana

Soma tena faida zitokanazo na karanga ili kupata manufaa zaidi ya siku 30 nzima za kusherehekea na kufurahia kila kitu kinachohusiana na siagi ya karanga.

Pika kwa Siagi ya Karanga Kwa kuzingatia jinsi siagi ya karanga inavyonyumbulika kama kiungo, Mwezi wa Wapenda Siagi ya Karanga ni fursa nzuri ya kuanza kuweka mboga hii ya jamii ya kunde katika vyakula na milo mbalimbali.

Kila siku weka lengo la kuongeza mlo mmoja wenye mada ya siagi ya karanga kwenye menyu ya kiamsha kinywa, chakula cha mchana au cha jioni.

Pius Vasco anatoa wito kwa serikali kuwawezesha mikopo yenye riba nafuu ili kuongeza uzalizaji wa zao hilo.

Shughuli za uchumi katika wilaya ya Bukombe ni Kilimo na ufugaji ambazo zinachukua asilimia 84 ya Mapato ya wakazi wote wa wilaya hiyo na asilimia 16 inahusisha shughuli za uchimbaji wa madini,biashara na,ufugaji nyuki.

Ikiwa ni kati ya Halmashauri sita zinazounda  Mkoa wa Geita, halmashauri hii inaushawishi wa kutosha kuweza kukumbuka shairi la “Karudi Baba Mmoja” kutokana na kuzungukwa na misitu kwa asilimia 60 na asilimia 40 ya eneo lote kufaa kwa makazi, Kilimo na Ufugaji.


Comments