TGNP Yalia na Udhalilishaji Wanawake


KUTOKANA na matukio ya udhalilishaji dhidi ya wanawake kuongezeka kwa kasi nchini, taasisi zinazotetea haki za wanawake na watoto, zimevitaka vyombo vya dola kuamka na kuchukua hatua za haraka zitakazosaidia kukomesha matukio hayo

Akizungumza jana na waandishi wa habari Dar es Salaam Lilian Liundi, Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia (TGNP), akiwa na wanaharakati wengine alisema kuwa, tangu Januari hadi kufikia Aprili mwaka huu matukio ya udhalilishaji na unyanyasaji dhidi ya wanawake yamekuwa yakizidi kushika kasi.

“Tuko hapa kwa pamoja tukilaani vikali ukatili dhidi ya wanawake unaoendelea kukithiri nchini, mfano kuna tukio lilitokea hivi karibuni katika mji mdogo wa Dakawa wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro ambapo binti wa miaka 21 alikuwa akibakwa na picha za video dhidi ya tukio hilo kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii,

“Si hilo tu bali taarifa tulizozikusanya juu ya matukio ya ukatili wa kijinsia tangu mwaka huu uanze ni mengi katika kila kona ya Tanzania, tunaona Aprili mwaka huu Yunis Peter mkazi wa Dar, alichomwa na kitu chenye ncha kali katika nyumba ya kulala wageni, Rehema Lubinza mkazi wa Mlele, aliuwawa kikatili kwa kukatwa na mapanga na mumewe kisha mwili wake kufungiwa ndani, si hivyo bali tukio la muuguzi wa Zahanati ya Kagu Geita, bi Elizabeth Msango, ambaye aliuwawa na watu wasiojulikanayapo matukio mengi ambayo ni unyanyasaji unaonekana kabisa”alisema.

Akizungumzia kuhusu udhalilishaji uliofanywa Mvomero, Gladness Munuo, Mratibu wa dawati la usuluhishi kutoka chama cha Wahariri Wanawake Tanzania, (TAMWA), alisema tukio hilo ni kinyume na sheria ya kanuni ya adhabu sura 16(Kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 ambayo imeainisha makosa ya kujamiana).

Alisema pamoja na sheria za ndani, serikali ya Tanzania imeridhia mikataba na matamko mengi kuhusu haki za wanawake na usawa wa kijinsia ikiwamo mkataba wa kutokomeza aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake(CEDAW), pamoja na mkataba wa haki za watoto (CRC), sambamba na tamko la kimataifa la haki za binadamu (UDHR,19),ambalo linatambua haki za wanawake na watoto.

Theodosia Nshala, Mkurugenzi wa kituo cha msaada wa sheria kwa wanawake (WLAC), alisema kama kituo tayari wameshapokea kesi kumi na mbili lakini licha ya kufanya jitihada za kuzishughulikia bado wahusika ama waathirika wamekuwa wakikata tamaa kutokana na kesi hizo kuchukua muda mrefu ambapo kesi moja ambayo ina ushahidi uliojitosheleza inaweza kuchukua hata miaka mitatu mpaka mitano .

Grace Mwangamila, Mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na haki za binadamu(LHRC), alisema kupitia tafiti zao matukio ya udhalilishaji dhidi ya wanawake yameoneka kuwa mengi huku kwa upande wa watoto udhalilishaji na unyanyasaji umebainika ukifanyika ndani ya familia.

Comments