SIKU 20 JIMBONI NA MAFUNZO YAKE; Na, Mh. Doto Mashaka Biteko (Mb)






Namshukuru Mungu  kwa Afya njema na kwa kuniwezesha kufanya ziara ya kulitembelea jimbo letu la Bukombe. Ziara hii imenichukua siku 20 ambapo nilitembelea kata 16 na kata moja mkutano wetu uliahirishwa  kutokana na msiba  uliojitokeza eneo  tulilopanga mkutano.
Nawashukuru sana wananchi wenzangu wa kata zote kwa mapokezi mazuri waliyonipatia  wakati wa ziara yetu. Nawashukuru pia kwa vikundi mbalimbali vya sanaa vilivyotumbuiza mikutano yetu, tumbuizo hizo pamoja kuburudisha mikutano yetu, ziliibua hoja za mjadala; kero mbalimbali zilitolewa kupitia kazi hizo za sanaa. Vyovyote vile wananchi kwenye kata tulizotembelea  walikaa kwetu mikutano toka mwanzo na hata mwisho wake.
Nawashukuru sana waheshimiwa Madiwani wetu wa kata zote pamoja na watendaji wetu wa kata na vijiji vyote tulivyovitembelea kwa kazi njema ya kuandaa mikutano hii tena kwa taarifa ya muda mfupi.
Nawashukuru pia wataalamu wote wa idara zote wa ngazi zote kwa kutusaidia sana kufafanua baadhi ya hoja za wananchi zilizojitokeza wakati wa kipindi cha ziara hii. Majibu yao  yalitupa msingi na mwelekeo wa ufahamu. Bila shaka wasingekua wao, mimi ningekua wa majibu yasiyo na uhakika ama yale yakusema ...”swala hilo nimelichukua ...” lakini walijibu kadri walivyoweza na kwa kiwango cha kuridhisha.
Mwisho nawashukuru wote tulioambatana pamoja kwenye ziara yetu Dereva wetu Shija  Malembela, katibu  wa mbunge ndg Benjamini Mugeta, Ndg Salum Mkadam Ndg Nelvin Sarabaga. Wote hawa waliifanya ziara yetu iwe rahisi.

YALIYOJTOKEZA
Sikuwahi kufikiri kama wananchi wa Bukombe  wana kiu ya maendeleo kwa kiwango kikubwa namna ile.
Ziara yetu ilikuwa na mahudhurio makubwa ya wananchi, aidha  wananchi kwa wingi walijitokeza  kuulizwa maswali mengi sana, ( hapa lazima nikiri) wengi walikosa nafasi ya kuuliza kwa sababu ya muda. Wote  waliopata nafasi waliuliza maswali ya msingi sana kwa manufaa ya wananchi wote bila kujali tofauti zao  (za kikabila, dini, upenzi wa vyama vya siasa n.k.) yaliyojitokeza ni mengi lakini hapa nitaelezea yaliyojitokeza kila mahali tulipofanya mkutano, kama ifuatavyo:-

1.   MAJI
Wilaya yetu ya Bukombe ipo nyuma sana kwa miradi ya maji. Miradi ya maji iliyopo wilayani kwetu ni ule wa kilimahewa, Msasa Runzewe Magharibi visima 8 (kwa juhudi ya Mhe. Diwani kupitia shirika la RUDDO), Bulega na Mradi wa uyovu.
Mradi wa Musasa ulishakufa, mradi wa Kilimahewa unafanyakazi chini ya kiwango, miradi ya uyovu mmoja tu unafanyakazi lakini mmoja wa kwa Mzibila  haufanyi kazi kutokana na ubovu wa pump. Bulega unafanya kazi ila wa Ibambilo haufanyi kazi.

Kwa kifupi sehemu kubwa ya wilaya yetu haina miradi sehemu nyingi ya maji, wananchi wanapata maji kutoka kwenye visima vya asili ambavyo haviwahakikishii usalama wa maji. Utaona ukweli kuwa Bukombe shida ya maji ni kubwa mno kuliko inavyoelezwa.

Wananchi wanatamani kuona kero hii inapunguzwa kwa haraka. Kazi hii ni ya serikali naamini kama mwakilishi wa wananchi ni kulisukuma kwa nguvu zote jambo hili ili tupunguze changamoto hii kubwa.

Kazi hii nitaianza, kuanzia Bunge la Bajeti lijalo linalotarajiwa kuanza tarehe 17/04/2016. Nawaomba wananchi wenzangu kuwa na subira wakati nikifatilia jambo hili nyeti na muhimu.

Aidha kwenye ngazi ya Halmashauri nawaomba na kuwasihi  madiwani tuanze kuibua miradi ya maji kwenye maeneo yetu. Hii itaisaidia serikali kupunguza gharama za utafiti. Nimeiomba pia halmashauri kuondoa mazingira yote, ambayo yanapelekea miradi kuwa  chini ya kiwango, mwisho wake fedha zinatumika ila wananchi hawapati maji. Imani yangu serikai nayo itaongeza msukumo wa kuleta miradi ya maji kwenye wilaya yetu. Katika ziara yetu jumla ya maswali 305 yaliulizwa mbapo katika hayo maswali 193 yalihusu  maji, kutokana na hali hii ni dhahiri suala la maji linawapa usumbufu mkubwa wananchi wetu.



2.   UMEME
Katika ziara yetu suala la umeme nimeulizwa mara nyingi zaidi kwenye kata zote. Wananchi waliuliza mikakati gani iliyopo ya kuwapatia umeme kwenye maeneo yao? Wapo pia ambao walitaka kujua waliopisha mradi ya umeme watalipwa lini fidia zao?

Umeme kwenye jimbo la Bukombe umetekelezwa kwa mradi wa umeme wa Electricity V. Mradi huu unatokana na mkopo wa fedha kutoka Benki ya maendeleo ya Africa (ADB) ambao, ulilenga kuvipatia umeme vijiji saba (7) tu wilayani kwetu ambavyo ni Ituga, Bukombe, Lyambamigongo, Ushirombo, Buntubili, Msasa na MJI wa Runzewe lakini kutokana na mahitaji ya umeme tulipeleka maombi maalumu tukaongezewa vijiji vingine 7 na kufanya  jumla ya vijiji 14 vitakavyonufaika na mradi wa elcticity V. Mradi huu umekamilika na sasa zoezi la usambazaji  ndilo linaendelea kwenye miji  ya ushirambo na Runzewe.

Kwakuwa wilaya yetu haikuwahi kupata umeme wa REA awamu zote mbili zilizopita. Sasa tumeomba nasi tuingizwe kwenye REA; nafurahi tumeingizwe kwenye mradi huu na tayari vijiji vyetu vyote 53 kwenye kata 17 zitapata umeme na utafikia zaidi ya vitongoji 176 kuanzia mwaka wa fedha ujao wa 2016/2017.

Kwakuwa uunganishwaji wa umeme ni ghari. Wizara imetuletea teknolojia mpya ambao mteja hatahitaji kuingia gharama ya kufanya wring kwanza ili kupokea umeme, chombo kiitwacho UMETA, hiki kitapunguza gharma kwa wananchi wetu ili wabakiwe na gharama ya kufungiwa mita mbayo ni shs 25,000/= tu na fomu ya maombi ni sh 6,000/=.
Imani yangu nikuwa wananchi nao watajipanga  kumudu gharama ya mita ili baada ya  muda nyumba zetu Bukombe ziwe zimepata na zinatumia huduma hii muhimu ya umeme.

Kuhusu fidia tunalifuatilia jambo hili kwa karibu tunafahamu wapo wananchi 258 wanadai  fidia mbalimbali za kupisha mradi wa umeme na wanadai 149,000,000 na zoezi la ulipaji linaendelea vizuri bila shaka malipo yataanza kulipwa kuanzia mwezi huu wa machi 2016.
Ninatoa wito kwa wananchi kutokuibua madai mapya nje ya yale yaliyothaminiwa, maana kufanya hivyo kunachelewesha upatikanaji na usambazaji wa umeme kwa watu wetu.

Wakati tunamalizia ziara, wafanyakazi wa TANESCO walifanya mkutano na wanachi wa uyovu kwenye mji wa Runzewe na kutoa taarifa kuwa watasambaza nguzo 25 tu. Jambo hili likizua manung’uniko mengi Niliamua kumwalika Naibu Waziri wa Nishati na Madini ambaye aliungana nasi kusikitika na hatimaye nguzo zimeongezwa kutoka 25 hadi 176. Hatua hii walau itafikia eneo kubwa zaidi la wananchi wa Uyovu na patakapo baki patamaliziwa na mradi wa REA.

Kwasasa nguzo zinaendelea kusambazwa Ushirombo na Uyovu ili kuwapatia umeme wananchi wengi zaidi.

3.   WACHIMBAJI WADOGO
Uchumi wa wilaya yetu umejengwa na uchimbaji wa dhahabu. Haishangazi kuona wanachi wengi zaidi wakiuliza juu ya wachimbaji wadogo.
Tumechukua hatua za kuleta suluhu  ya kudumu kwa wachimbaji wetu. Mazumgumzo tumefanya na mgodi wa STAMIGOLD wa Tulawaka Biharamulo ili waachie sehemu ya leseni zao ambazo hawazifanyii kazi   tuwapatie wananchi (wachimbaji wadogo wadogo) waweze kuendesha shughuli zao.

Sisi wabunge wa Bukombe na Biharamlo tulifanya kikao  na uongozi wa mgodi kwa siku mbili tarehe 17/02/2016 na 18/02/2016 mbapo tulikubaliana kulipa msukumo jambo hili. Tayari tumeshawasiliana na wizara juu ya makubaliano yetu wizara imeyapitia mapendekezo yetu bila shaka utaratibu wa namna gani utatolewa  zoezi hili litekelezwe zaidi kwaajili ya watu wetu.

Wito wangu kwa wachimbani wadogo sasa wafikirie kujiunga kwenye vikundi ili umilikishaji ukianza tuwe na mazingira mazuri ya kuanza kazi badala ya maandalizi.

Naibu waziri pia alipotutembelea pale Uyovu alituhakikishia anaenda kulifanya kazi kwa haraka ili kazi ianze mapema.

Ninatoa wito kwa wananchi kuwa na subira wakati tukilifuatilia jambo hili.


4.   ELIMU
Masuala ya elimu pia yaliulizwa na kwakweli yalitupa mwanga kuwa mwamko wa elimu wilayani kwetu unakuwa kwa kasi zaidi. Tumebaini mengi sana ya uelewa naya kufanyia kazi.

Masuala ya uhaba wa walimu wa shule za msingi ambapo wilaya yetu inaupungufu wa walimu 436, hata hivyo idadi inaweza kuongezeka zaidi kutokana na idadi kubwa zaidi ya wanafunzi wa darasa la kwanza kuandikishwa kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko matarajio yetu kutokanana mwitikio wa elimu bure.

Kwenye shule za sekondari pia kwa uhaba wawalimu wa sayansi; shule nyingine hazina hata mwalimu mmoja wa sayansi; tunapambana kuleta walimu wengine  kwenye ajira ya walimu ijayo.

Elimu bure imezaa changamoto za upungufu wa madarasa na madawati. Shule ya Ibamba ndiyo inayoongoza kwa mkoa wa Geita kwa kuandishaji watoto wengi zaidi ambapo zaidi ya watoto 1800 wameandikishwa.

Uwepo wa changamoto hizi lazima tufikiri zaidi namna ya kuzitatua, tunaamini tutaendela kuboresha kadri tunavyoendea.
Walimu wetu wanamadai yao,  ambayo kwa muda mrefu hayajafanyiwa kazi, mathalani:-
a.    Madai ya kutokupandishwa madaraja kwa wakati
b.    Kutorekebishiwa mishahara yao kwa wakati na malimbikizo ya mishahara yao kutokulipwa kwa wakati
c.    Walimu wapya kutokupatiwa namba zao za ajira TSD numbers pamoja na vitambulisho vya kazi hawajapatiwa
d.    Kada hii haijapata motisha yoyote toka kwa mwajiri
e.    Wapo walimu waliopelekwa kwenye  mifuko ya hifadhi ya jamii ambayo si machaguo yao.
Baada ya ziara hii yapo ambayo kwa haraka tuliamua kuyachukulia hatua.

Upandishwaji  wa madaraja, tuliwasiliana na ofisi  husika na wataanza kupandishwa waliogota muda mrefu wapo walimu 145 tu watakao pandishwa kwa sasa.

Namba za TSD tumewaomba wazifuate mkoani haraka na tayari zitaanza kusambazwa wiki ya pili ya mwezi machi.

Ama kuhusu motisha, tunafanya mazungumzo na makampuni ambayo yanaweza kuwakopesha walimu vyombo vya usafiri. Imani yangu  hilo likifanikiwa litatupa hatua zaidi kwa walimu na watumishi wengine.

Tumeitaka ofisi ya utumishi ipeleke haraka watumishi kwenye mifuko waliyochagua, bila shaka hilo litatekelezwa mapema.

5.   MALI ASILI
Wananchi wengi wanokaa kando kando ya hifadhi wametoa malalamiko mengi juu ya mahusiano mabaya kati yao (wananchi) na wahifadhi wa misitu  na maliasili nyingine kwenye pori la kigosi. Kuna taarifa za watu wanaotozwa mamilioni ya fedha kama rushwa, wanapigwa, wapo wamepata ulemavu na wengine wamenyang’anywa mali zao.

Tumeyapokea na kwakweli tunalaani sana unyanyasaji unaofanywa  kwa wananchi, wahifadhi wanapaswa kufuata sheria ingawa watekelezaji wa sheria wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kufuata sheria pia.
Vitendo vya kuomba rushwa, kupiga wananchi na unyang’anyi wa mali za wananchi si utekelezaji wa sheria  bali ni wizi na “uhuni’ kama uhuni mwingine

Tumeomba waziri wa maliasili utalii atembelee jimbo letu ili  nae asikie mwenyewe manyanyaso haya kwa  wananchi.

6.   MILIONI HAMSINI ZA WANAWAKE, VIJANA ZA KILA KIJIJI.
Suala hili limeulizwa sana, walau swali moja kwa kila makutano liliulizwa juu ya upatikanaji wa fedha hizo

Ahadi hii itatekelezwa na kuanzia mwaka ujao wa fedha 2016/2017 serikali italeta utaratibu wa namna gani fedha hizo zitapatikana  tumewaomba wananchi na hasa akina mama wawe na subira wakati jambo hili linafanyiwa kazi.

7.   TOZO ZA MAFUNDI SELEMALA.
Mafundi selemala kwenye wilaya yetu; wana malalamiko mengi juu ya tozo kubwa zinazodaiwa na Halmashauiri mfano. Kitanda kimoja kinatozwa hadi shs 120,000 kiasi hiki ni kikubwa  mno, ukilinganisha na uwezo wa wateja wao.
Bahati njema hata mkuu wa mkoa nae alishalifanyia kazi kwa kulitolea maelekezo ya kupunguza gharama hizo.

8.   KILIMO NA UFUGAJI
Wakulima wetu hasa wa pamba, hawajafurahishwa na kilimo cha mkataba. Kilimo cha mkataba kimesababisha bei ya mazao  yao haipandi na kwamba pembejeo haziletwi kwa wakati.

Kikao cha RCC kilichoketi kilielekeza ununuzi wa pamba utakapoanza kila mnunuzi apate nafasi sawa ya kununua, mfumo wa msimu uliopita hatatumika tena isipokua kwa wakulima walioingia wenyewe kwenye mikataba.

Wafugaji kama ilivyo sehemu nyingine hapa nchini wafugaji hawana maeneo ya kulishia mifugo suala hili tutaendelea kulifanyia kazi, kitaifa na kiwilaya ili tutoe ahueni kwa wafugaji wetu.

9.   Huduma za Afya
Wananchi wengi kwenye mikutano yetu wameomba uwepo wa huduma za Afya karibu zaidi na wao, aidha wanasikitishwa sana ukosefu wa madawa kwenye vituo vya kutolea huduma.

Nimewaomba watuvumilie tunalifanyia kazi maana pamoja na kua limeibuka jimboni ni tatizo hili limekua kila mahali hapa nchini. Tunaenda kwenye bajeti tutalisema kwa nguvu zote.


                                                HITIMISHO
Siku 20  jimboni zimenipa somo, zimenipa picha ya kila kinachoendelea jimboni. Nimewaona mama zangu, baba zangu na ndugu zangu na dada zangu ambao wana kiu ya haki ya maendeleo. Wananachi wanatamani kero hizi ziondoshwe, wanatamani maisha bora kupitia raslimali ambazo Mungu aliwapa, wanatamani wapate majawabu ya kero hizo!

Wananchi wamenipa somo kuwa kama mbunge wajibu wa mbunge ni kuwa sauti ya wananchi na daraja kati yao na serikali, nami kama mbunge nitahakikisha muunganiko huo unakuwepo wakati wote.

Binafsi kama mbuge, nitaendelea kuwa na wanabukombe wakati wote. Nawasihi waendelee kunipa ushirikiano nitawaambia ukweli tupu. Na waniombee nami nitawaombea, ili pamoja tujenge Bukombe yetu.

Kusema na kutenda, uwe Msingi Wetu Sote.




Comments