DKT. BITEKO AWATAKIA EID MBARAKA WATU WA BUKOMBE

Na, Ernest Magashi

Mbunge wa Jimbo la Bukombe mkoani Geita, Naibu Waziri Mkuu mstaafu, Dkt. Doto Biteko, amewatakia heri ya Sikukuu ya Eid wananchi wa jimbo hilo pamoja na waumini wa dini ya Kiislamu nchini.
Akitoa salamu zake za Eid, Dkt. Biteko amewaomba wananchi kusherehekea sikukuu hiyo kwa amani, upendo na kuendelea kudumisha mshikamano pamoja na umoja wa kitaifa.
Aidha, amesema ni vyema kwa waumini kuyaishi mafundisho waliyojifunza wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani ili kuimarisha upendo, mshikamano na amani ya nchi.
Kwa upande wake, mkazi wa Bukombe, Selemani Juma, ambaye ni muumini wa dini ya Kiislamu, amesema anashukuru kufikia siku ya Eid na kusherehekea pamoja na waumini wenzake. Ameongeza kuwa anakumbuka tukio la Machi 16, 2026, aliposhiriki futari iliyoandaliwa katika Uwanja wa Mwenge, Kata ya Uyovu, na Mbunge Dkt. Biteko, ambayo iliwaunganisha wananchi wa dini mbalimbali.
Naye Adija Haluna amesema amepokea salamu za Eid kutoka kwa Mbunge huyo kwa furaha, na ameahidi kuendelea kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ili aendelee kubarikiwa na kupewa afya njema katika kuwatumikia wananchi.

Comments