MAWAZIRI WA NISHATI WA TANZANIA, RWANDA NA BURUNDI WAKAGUA MRADI WA UMEME WA RUSUMO (MW 80)


✅️MRADI WAFIKIA ASILIMIA 99.7


✅️MTAMBO MMOJA KATI YA MITATU WAWASHWA


Mawaziri wa Nishati kutoka nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi  wakiongozwa na Mwenyekiti wa Mawaziri hao, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko leo wamefanya kikao cha ngazi ya Mawaziri na kukagua mradi wa umeme wa Rusumo utakaozalisha megawati 80 na kila nchi itapata megawati  27.


Akizungumza na waandishi wa habari tarehe 30 Septemba, 2023, katika eneo la mradi, wilayani Ngara Mkoa wa Kagera, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko amesema kuwa, mradi huo ni wa kihistoria na kukamilika kwake kutapelekea ongezeko la umeme kwa nchi zote tatu. 


"Leo tumewasha mashine moja ya kuzalisha umeme na mashine mbili zilizobaki zitawashwa mwezi Oktoba mwaka 2023 tunawashukuru sana Marais wa nchi zote tatu kwa kuhakikisha kuwa mradi huu unatekelezwa  pamoja Benki ya Dunia (WB) na Benki ya Maendeleo Africa (AfDB) kwa kuchangia fedha zilizowezesha mradi huo kutekelezeka." Amesema Dkt. Biteko



Amesema kuwa, kukamilika kwa mradi huo kutakuwa na manufaa mengi kwa nchi ikiwemo kuongeza megawati 27 katika gridi ya Taifa na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika mikoa ya Kagera, Geita na Kigoma na pia   kuchochea uwekezaji katika viwanda na kukuza uchumi wa wananchi.


Ameongeza kuwa, mradi wa Rusumo pamoja na kuhusisha miundombinu ya kuzalisha umeme na kusafirisha umeme wa msongo wa kV220, mradi huo pia umehusisha kujenga miradi ya kijamii ya shilingi bilioni 25  inayojumuisha ujenzi wa kituo cha Afya Rusumo na Lukole ,mradi wa maji Rusumo, madarasa na mabweni na maabara katika shule za msingi na sekondari pamoja na  kuendeleza wananchi katika miradi ya kilimo na ufugaji.


Kuhusu uzinduzi wa mradi huo amesema kuwa utazinduliwa mwezi Desemba mwaka 2023 ambapo inatarajiwa kuwa viongozi wakuu wa nchi zote Tatu watauzindua.



Viongozi wengine kutoka Wizara ya Nishati waliohudhuria kikao hicho ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga.




Comments