DKT. BITEKO ASISITIZA WADAU KUSHIRIKI KONGAMANO LA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI 2023

 


Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko ametoa wito kwa wadau wote wa madini wa ndani na nje ya nchi kushiriki katika Kongamano la Kimataifa la Uwekezaji katika Sekta ya Madini linalotarajiwa kufanyika Oktoba 25 na 26, 2023.


Ametoa wito huo katika hafla fupi iliyozikutanisha Kampuni mbalimbali zilizowekeza nchini hususan katika Sekta ya Madini iliyo fanyika Juni 02, 2023 jijini Dar es Salaam.  


Aidha, Dkt. Biteko amesema Australia ni Taifa la mfano na lenye kupaswa kuigwa katika uwekezaji wa Sekta ya Madini ambalo lina uzoefu mkubwa katika shughuli za uwekezaji wa madini.


“Hivi karibuni Taifa limeshuhudia utiaji saini mikataba ya uchimbaji mkubwa na wa kati wa madini muhimu ya Kinywe na Rare earth element wenye thamani za dola za Marekani Milioni 667 kwa  Kampuni tatu  kutoka nchini Australia,” amesema Dkt. Biteko. 


Pamoja na mambo mengine, Dkt. Biteko amesema lengo la Tanzania ni kutoa mchango mkubwa  katika mnyororo mzima wa upatikanaji wa madini muhimu ulimwenguni kwa lengo la kuiokoa dunia katika mabadiliko ya hali ya hewa.



Pia, amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na Australia katika nyanja mbalimbali hususan katika uchimbaji na uchenjuaji wa madini ili kuongeza tija katika sekta hiyo.


Sambamba na hayo, Dkt. Biteko amesema Serikali itaendelea kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wadau wa Sekta ya Madini ili kuiwezesha sekta hiyo kuchangia asilimia 10 ya Pato la Taifa ifikapo Mwaka 2025 ambapo mpaka sasa mchango wa sekta hiyo kwenye Pato la Taifa umeongezeka na kufikia asilimia 9.7.


Comments