SHILINGI BIL. 89.3 ZAPITISHWA NA BUNGE KWA WIZARA YA MADINI

 *



*

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha Bajeti ya jumla ya shilingi 89,357,491,000.00  kwa ajili ya Matumizi ya Wizara na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024.


Kati ya fedha hizo, Shilingi 23,172,550,000.00  ni kwa ajili  ya shughuli za  maendeleo, Shilingi 66,184,941,000.00 kwa  ajili ya Matumizi ya Kawaida. Kati ya fedha hizo, shilingi 20,307,498,000.00 ni kwa ajili ya Mishahara na shilingi 45,877,443,000.00 ni Matumizi Mengineyo.



Akiwasilisha hotuba yake bungeni Aprili 27, 2023, Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko alisema  Wizara inatarajia kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia vipaumbele vyake na kuvitaja kuwa ni pamoja na kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa; Kuendeleza madini muhimu na madini mkakati; kuwaendeleza na kusogeza huduma za ugani kwa wachimbaji wadogo.



Alivitaja vingine kuwa ni pamoja na kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini; kuhamasisha uwekezaji na biashara katika Sekta ya Madini, uanzishwaji wa minada na maonesho ya madini ya vito; na kuzijengea uwezo taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini ili ziweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.


Akizungumzia  namna wizara ilivyojipanga kuendeleza madini  muhimu na mkakati yanayohitajika kwa kiasi kikubwa kwa sasa duniani, amesema katika kuendeleza madini muhimu na madini mkakati (critical and strategic minerals), Wizara imepanga kufanya tafiti na kutangaza fursa za madini mkakati na muhimu zilizopo; kuhamasisha uwekezaji katika utafutaji na uchimbaji wa madini mkakati na madini muhimu; kutoa leseni za utafutaji, uchimbaji na biashara ya madini mkakati na madini muhimu; na kuandaa Mpango Mkakati wa Uendelezaji wa shughuli za uchimbaji wa madini mkakati nchini.


Aidha, Dkt. Biteko alisema miongoni mwa madini mkakati ambayo yatapewa kipaumbele katika utafiti ni pamoja na madini ya kinywe, nikeli, rare earth elements, cobalt, lithium, manganese, vanadium, niobium, titanium na tin.



‘’Mhe. Spika Madini haya yanahitajika kwa kiasi kikubwa kwenye vifaa vya kielektroniki, betri za magari yanayotumia nishati ya umeme, vifaa vya ndege na vyombo vingine vinavyoruka angani, vifaa vinavyozalisha nishati ya umeme kupitia upepo na mwanga wa jua, na vifaa vya kisasa vinavyotumika katika kulinda usalama wa nchi,’’ amesema Dkt. Biteko.


Ameongeza kwamba, mpango wa muda wa kati na mrefu ni kuyatumia madini hayo kuzalisha bidhaa au teknolojia mbalimbali hapa nchini.



Wakichangia hoja, wabunge wameitaka wizara kujiandaa kikamilifu kuhakikisha taifa linanufaika ipasavyo na rasilimali hiyo inayohitajika sana duniani ikiwemo nchi kushiriki kwenye uwekezaji wa madini hayo.


Naye, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akijibu hoja  amesema  wizara imetanua uwanda wa uwekezaji na kuweka msukumo kwenye madini mkakati na kuongeza kwamba  imejipanga kuhakikisha kila kinachogundulika kinajulikana ili taifa linufaike.

Comments