KAMATI YA BUNGE YAPITISHA RANDAMA KWA WIZARA YA MADINI NA TAASISI ZAKE



Kitandula aipongeza wizara kwa kuwasilisha vipaumbele vya mwaka 2023/24 vinavyotekelezeka

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepitisha Maelezo ya Randama kuhusu Makadirio ya Mapato, Matumizi ya kawaida na maendeleo kwa wizara na taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2023/24.


Kamati hiyo imepitisha Randama hiyo leo Machi 29, 2023 kwenye kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Pius Msekwa C Jijini Dodoma kilichohusisha Wizara ya Madini na Taasisi zake.



Akizungumza kwenye kikao hicho, Mwenyekiti wa kamati hiyo Danstan Kitandula ameitaka Wizara ya Madini na Taasisi zake kuzingatia maelekezo yote yaliyotolewa na kamati hiyo ili  kuiwezesha wizara kufikia lengo la makusanyo lililowekwa na Serikali.


Aidha, Kitandula amesema kamati anayoiongoza imepokea taarifa za utekelezaji na vipaumbele vya wizara na taasisi zake ambapo ameipongeza Wizara hiyo kwa kuweka vipaumbele muhimu ambavyo vinatekelezeka.



Kwa upande wake, Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko amesema Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2023/24 umeandaliwa kwa kuzingatia miongozo mbalimbali ya Kitaifa ikiwa ni pamoja na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2023/24, Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2025, Sera ya Madini ya Mwaka 2009 na maelekezo ya Rais.


Pia, Dkt. Biteko amesema fedha zinazoombwa kuidhinishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mwaka Fedha 2023/24 ni kwa ajili ya matumizi ya Wizara na Taasisi zake ikiwemo miradi ya maendeleo, mishahara ya watumishi, matumizi ya mengineyo.


Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Madini Kheri Mahimbali ameipongeza kamati hiyo kwa usimamizi na maelekezo mazuri inayoyatoa kwa wizara hiyo ambapo ameahidi kuyazingatia maelekezo yote yaliyotolewa na kamati hiyo.


"Napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru kamati hii kwa maelekezo mazuri inayotupatia na nipende kuahidi kwamba sisi kama Wizara ya Madini tutayafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na kamati hii", amesema Mahimbali.

Comments