WAZIRI BITEKO ATAJA VINARA UTOROSHAJI DHAHABU GEITA

Atoa siku 30 kwa mgodi wa dhahabu Geita kulipa fidia wananchi walioathirika na shughuli za uchimbaji za mgodi huo

Waziri wa Madini, Doto Biteko  ametaja majina matatu ya wafanyabiashara  wakubwa wa dhahabu (Dealers) wanaoshiriki  katika vitendo vya  utoroshaji Dhahabu ndani ya Mkoa wa Geita.


Ametaja majina hayo kuwa ni mfanyabiashara wa Dhahabu Maduka Mbaraka, Makandaga Sita na Makaranga Kiserya.



Ametaja majina  hayo leo Desemba 29, 2020 alipofanya ziara na kutembelea Soko la Madini la  Mkoa wa Geita, pamoja na kukutana na kuzungumza na Wafanyabiashara Wadogo  (Brokers) na Wafanyabiashara wakubwa wa Madini (Dealers) katika ukumbi wa Mwalimu nyerere katika Kituo cha uwekezaji cha mjini Geita (EPZA) na kuwataka kutojihusisha na utoroshaji wa madini nchini.


Amewaeleza  kuwa, tayari amepata majina 

ya wafanyabiashara wa madini sita katika mkoa wa huo wanaosifika kwa utoroshaji wa Madini lakini  ameamua kutaja majina matatu kwanza na mengine matatu  ameyahifadhi .


Amesema wafanya biashara hao wananunua Dhahabu nje ya masoko na kuuza kusikojulikana kinyume na sheria zinazosimamia sekta ya madini nchini.



Ametoa onyo la mwisho kwa wafanyabiashara hao na kuwataka  wajirekebishe vinginevyo  hatua kali zinatachukuliwa dhidi yao ikiwemo kuwafilisi Mali zao pamoja na kuwafikisha mahakamani.


"Ninawaomba tuheshimu taratibu zilizowekwa na Serikali katika kusimamia Sekta ya Madini, ifike kipindi tuone fahali kulipa Kodi. 


Amebainisha kuwa,  kwenye Maonyesho ya Madini 

Yanayotegegemewa kuyafanyika Mwaka 2021 tunzo  kwa Wafanyabiashara  wanaofuata utaratibu mzuri wa kulipa Kodi zitatolewa na kuwataka kujiandaa kwa kufuata taratibu na kanuni zilizowekwa.



Amesema kuwa Rais Dkt.John Magufuli aliwafutia Kodi na tozo nyingi  za madini ambazo zilizofikia takribani asilimia 21 ili waweze kufanya biashara hiyo pasipo  kutorosha madini.

Aidha, Biteko ametaja kiwango Cha Kodi wanacholipa kwa mujibu wa sheria kuwa ni asilimia Saba pekee, kiwango ambacho ni rafiki kwa kila mfanyabiashara wa madini.

"Tukikukamata unatorosha Madini, tunachukua leseni, nadhani mmeona yaliyotokea Chunya tumefuta leseni sita na Wilaya ya Kahama leseni 4". Amesisitiza Biteko."



Pamoja na hayo, Waziri Biteko amewataka wafanyabiashara hao wasioneane wivu wa kibiashara kwa kuwasingizia wengine  kuwa wanahusika na utoroshaji baada ya kuona mwenzao wanafanya vizuri badala yake watoe taarifa sahihi na zenye ukweli ili wale wanaokiuka taratibu wachukuliwe hatua.

Katika hatua nyingine Waziri wa Madini  Biteko,ameagiza wafanyabiashara wadogo wa Dhahabu (Brokers) kununua dhahabu bila kuzuiliwa kwa kuwekewa matabaka ya Dhahabu inayotoka kwenye viwanda vya kuchenjua Dhahabu ( Elution plant) na inayotoka kwenye mialo .


Agizo hilo limekuja baada ya mfanyabiashara Charles Kazungu kulalamikia utaratibu wa kuzuia wafanya biashara hao kununua dhahabu inayotoka kwenye vinu vya kuchenjulia badala yake wameelekezwa wanunue inayotoka kwa mchimbaji mdogo anayepata Dhahabu kwa kukamatisha kwa Zebaki .


Biteko amesema Sheria inamruhusu mfanyabiashara  mdogo kununua dhahabu yoyote na kiwango chochote ilimradi hawezi kuuza nje ya nchi.


Aidha ,Waziri Biteko ametoa siku 30 kwa mgodi Mkubwa wa uchimbaji wa madini ya Dhahabu wa Geita (GGML) kulipa fidia wananchi 1,200 ambao nyumba zao zimepasuka kutokana na shughuli za uchimbaji zinazo fanywa na mgodi huo.



Naye, Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel amempongeza Waziri wa Madini Doto Biteko kwa kuisimamia vizuri Sekta ya Madini.


 Mhandisi Gabriel ameahidi ushirikiano baina yake na  Waziri Biteko katika katika kusimamia Rasilimali Madini kwa mkoa wa Geita.


Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Geita mjini Constantine Kanyasu amepongeza uamuzi wa Waziri Biteko kuchukua hatua kali dhidi ya wafanyabiashara wanaotorosha madini kwani wanahujumu mapato ya serikali.


Ameongeza kuwa, kitendo Cha kutoa siku 30 kwa GGML kulipa fidia wananchi 1200 wa mitaa inayozunguka mgodi huo ambayo nyumba zao zilipasuka ,ni Jambo la muhimu na kutaka mgodi huo kuheshimu maagizo hayo.


Amesema siku za nyuma mgodi huo ulisingizia mlipuko wa ugonjwa wa covid -19 lakini Sasa hivi ni muda muafaka kuwalipa wananchi hao.


Waziri wa Madini Doto Biteko Yuko mkoani Geita kwa  ziara ya siku mbili ili  kukutana na kusikiliza kero za wadau wa  madini ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara na wachimbaji wa madini.



Comments