Waziri wa Madini, Doto Biteko amewataka watanzania kuutazama mchango wa sekta ya madini kwa namna unavyosaidia kuinua sekta nyingine za uchumi  kwani tayari kwa upande wa kuongezeka kwa ukusanyaji wa maduhuli sekta hiyo imeonesha mafanikio makubwa.

“Niliwaambia wenzangu wizarani, lazima tuhame sasa kwenye mfumo wa kufurahia kuona mapato yameongezeka kutokana na ukusanyaji wa maduhuli twende kwenye mfumo wa kujiuliza je? sekta ya madini imechangiaje ukuaji wa sekta nyingine?” alisisitiza.

Amesema anayelima mchele awe na uhakika wa wanunuzi kwa sababu wachimbaji wapo, anayefuga ng’ombe awe na uhakika wa soko kwa sababu wanunuzi wapo, anayelima nyanya na shughuli nyingine hivyohivyo, na huo ndio tunaita ufungamanishaji wa uchumi wa madini na sekta nyingine”. Biteko alisisitiza.

Kauli hiyo ameitoa tarehe 4 Juni, 2020 mkoani Geita alipofanya ziara ya kutembelea miradi ya maendeleo inayofanywa kwa fedha za huduma za jamii (CSR) zinazotolewa na Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) ambapo alikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo jipya unaoendelea katika soko kuu la dhahabu Geita pamoja na soko la Katundu litakalohusisha biashara za kawaida lililojengwa katika halmashauri ya mji wa Geita.

Pamoja na kukagua miradi ya maendeleo inayowezeshwa na GGML, Waziri Biteko alizungumza na wafanyabiashara wa madini mkoani humo na kueleza kuwa kutokana na changamoto ya covid 19, wizara imetoa kipindi cha miezi mitatu kwa wafanyabiashara wa madini kununua madini mahala popote nchini na kuwataka kuzingatia uwepo wa vibali vyote muhimu vinavyoonesha mahala madini hayo yamenunuliwa na yanakopelekwa mara baada ya kuyanunua.

Akitoa taarifa ya sekta,  Mkuu wa Mkoa wa Geita, Robert Gabriel amesema mwenendo wa biashara ya madini ya dhahabu katika Mkoa wake tangu soko la dhahbu kufunguliwa mwezi Machi 2019 hadi Mei 2020 kipindi cha miezi 14 jumla ya kg 5,320.99 zenye thamani shilingi Bilioni 522.44 zimeuzwa na kuchangia mapato ya serikali kupitia  mrabaha na ada ya ukaguzi kwa jumla ya shilingi bilioni 36.57.

Amesema ongezeko hilo linaonesha namna sekta ya madini ilivyokuwa na mafanikio makubwa sana kutokana na usimamizi makini na uongozi bora wa wizara lakini pia utii na utekelezaji wa ushauri na maelekezo yanayotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Aliongeza kusema fedha inayopatikana kutokana na makusanyo kwenye sekta ya madini ndiyo inayokwenda kulipa elimu bure, kujenga vituo vya afya, inatumika katika kujenga hospitali za wilaya na mambo mengine mengi yanayotekelezwa na serikali yetu.

Amebainisha  kuwa, Mkoani Geita kuna ongezeko kubwa la viwanda vya kuchenjua dhahabu  (Illusion Plant) kutoka viwanda 20 vilivyokuwepo awali na kufikia viwanda 39 na kubainisha kuwa  hayo ni mageuzi makubwa katika sekta ya madini kwa kuwezesha uwepo wa viwanda vidogovidogo mkoani humo.

Ameendelea kusema kwa mwaka 2018  halmashauri zilizoko katika Mkoa wa Geita zilinufaika kutokana na utekelezaji wa takwa la kisheria la utekelezaji wa mpango wa kuchangia huduma za kijamii ambapo Mgodi wa Geita (GGML) uliotoa kiasi cha shilingi bilioni 9.2 kama mchango wa Mgodi kwenye masuala ya kijamii na kupelekea maendeleo ya mkoa huo kwenda kwa kasi.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, Mjiolojia Daniel Mapunda amesema, Mkoa wa Geita una leseni kubwa za utafiti wa madini 283, leseni za uchimbaji mkubwa wa madini 2, leseni 17 za uchimbaji wa kati, leseni 1487 za uchimbaji mdogo wa madini na leseni 384 za uchenjuaji wa madini (illusion plant na vat-reaching plant).

Kwa upande wa leseni za biashara ya madini, Mapunda amesema kuna jumla ya leseni kubwa za biashara ya madini 33 kwenye soko kuu la dhahabu Geita na leseni ndogo za biashara ya madini 69 zilizopo katika vituo vidogovidogo vya ununuzi wa madini zilizotolewa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020.

Akizungumzia mwenendo wa ukusanyaji wa maduhuli ya serikali, Mapunda ameeleza kuwa lengo la makusanyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020 lilikuwa ni kukusanya shilingi bilioni 156.34 ambapo kufikia tarehe 2 June, 2020 kiasi cha shilingi bilioni 191.52 sawa na asilimia 122.5% ya lengo la makusanyo kimekusanywa.

Amesema makusanyo hayo ni ongezeko la kiasi cha shilingi bilioni 62.54 ukilinganisha na kiasi kilichokusanywa kwa mwaka wa fedha 2018/2019 . Amebainisha kuwa, kati ya hizo jumla ya shilingi bilioni 34.2 zimetokana na shughuli za uchimbaji mdogo wa madini sawa na ongezeko la asilimia 310 ya mapato yaliyopatikana kutokana na uchimbaji mdogo kwa mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo kiasi kilichokusanywa ni shilingi bilioni 11 pekee.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Makamu wa Rais anayeshughulikia Miradi Endelevu (GGML) Simon Shayo, alisema kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni 9 kilitolewa kwa mwaka 2018 ili kuzinufaisha jamii zinazozunguka mgodi huo na kuongeza kuwa mgodi unafurahi kuona wananchi wa kawaida wakiboresha maisha yao kutokana na mgodi kuwepo katika jamii yao.

Katika ziara hiyo, Waziri wa Madini alikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo jipya litakalohusisha wafanyabiashara wengine wa dhahabu katika soko la dhahabu Geita, ujenzi wa soko la Katundu, kukagua kituo cha uwekezaji Bombambili, pia alikagua maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha kuchakata madini kinachojengwa na mwekezaji binafsi mkoani humo.


Comments