Skip to main content

Wizara itaendelea kuanzisha masoko ya madini-Biteko


Wizara itaendelea kuanzisha masoko ya madini-Biteko

Imeelezwa kuwa, Wizara ya Madini itaendelea kusimamia Uanzishwaji wa Masoko ya Madini katika maeneo mbalimbali nchini huku ikiendelea kufanya marekebisho ya Kanuni za Uanzishwaji wa masoko hayo.
Waziri wa Madini Doto Biteko ameysema hayo Machi 31, 2019 wakati akifunga Semina ya siku mbili iliyoandaliwa na wizara kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini pamoja na baadhi ya Wenyeviti wa Kamati zenye uhusiano na Sekta ya Madini.
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya Wenyeviti wa Kamati nyingine wakifuatilia uwasilishaji wa mada uliotolewa na Wataalam kutoka Wizara ya Madini na Taasisi zake.
Semina hiyo ililenga kutoa elimu na kujenga uelewa wa pamoja kwa wabunge hao kuhusu sekta ya madini ambapo mada mbalimbali ziliwasilishwa.
Mada zilizowasilishwa ni pamoja na uanzishwaji wa masoko ya madini, mafanikio na changamoto ya Shirika la Madini la Taifa STAMICO), elimu kuhusu majanga ya asili (hasa matetemeko ya ardhi), ukaguzi migodini, biashara ya madini na shughuli zinazofanywa na Taasisi ya Uwazi na uwajibikaji katika Rasiimali za Madini, Mafuta na Gesi Asilia.
Waziri Biteko aliongeza kuwa, Wizara itaendelea kuwaelea wadau wa madini huku akiwataka kubadilika na kutenda matendo yenye manufaa kwa pande mbili na kuwaomba wabunge hao kushirikiana na serikali katika kutoa elimu kwa wadau wa madini ili waweze kuzingatia na kufuata taratibu zilizowekwa.
Pia, alisema serikali itaendelea kufanya kaguzi migodini kwa lengo la kuhakikisha wachimbaji wanachimba kwa usalama na kueleza kuwa, wizara imeomba kibali cha kuongeza maeneo mengine ya ukaguzi wa madini na kusema,“ tumepanga kuongeza vituo vingine 85”.
Aidha, alizungumzia maeneo yenye wizi wa dhahabu katika maeneo ya kuchanjua madini hayo na kuyataja kuwa ni Kahama na Chunya na kuwataka wahusika kuzingatia sheria.
Akizungumzia suala la kupunguza zaidi kodi kwa uchimbaji mdogo wa madini, alisema serikali haitapunguza tena kodi hizo kwa sasa mpaka hapo itakapoona manufaa yake.
Ikumbukwe kuwa, baada ya mkutano wa Kisekta uliofanyika Januari 22 mwaka huu chini ya Uenyekiti wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli na kuwashirikisha wadau mbalimbali wa madini baada ya wadau hao kuwasilisha kero zao kubwa ikiwa kodi, serikali ilifanya mabadiliko na kuondoa kodi kwenye uchimbaji mdogo wa madini kwa kuwafutia kodi ya ongezeko la thamani yaani VAT  (18%) na  kodi ya zuio( withholding tax).
Mbali na wajumbe wa kamati, wengine walioshiriki semina hiyo ni Wenyeviti wa Bodi za Taasisi zilizo chini ya Wizara pamoja na Watendaji na Wataalam kutoka wizara na taasisi zake.

Comments