Ukuta wa Mirerani sababu ongezeko la Mapato




Waziri wa Madini Doto Biteko amewamwagia sifa Wachimbaji na Wafanyabiashara wa Madini ya Tanzanite mkoani Manyara kwa kuongeza mchango wao kwenye pato la Taifa.
Biteko ametoa pongezi hizo leo wakati wa Mkutano baina ya wachimbaji na wafanyabiashara hao pamoja na viongozi wa Wizara ya madini na Tume ya madini uliofanyika wilayani Sumanjiro,  mkoani Manyara.
Miaka iliyopita tulikuwa tunakusanya milioni 60 hadi milioni 70 kwa mwaka lakini tokea tumeujenga ukuta huu, mapato yameongezeka mpaka kufikia makusanyo ya billion 2.1 kwa mwaka ambapo ni ongezeko kubwa sana hivyo nawashukuru sana watu wote wanaofanya shughuli zao hapa Mirerani.
Biteko aliongeza kuwa, ameamua kufanya mkutano huo akiambatana na viongozi waandamizi wa wizara ya Madini pamoja na Tume ya Madini ili nao pia wasikie maagizo ninayotoa na waanze kuyafanyia kazi badala ya kurudi na kuitisha kikao kingine ofisini.
Akizungumza manufaa ya ukuta huo kwa wakazi wa Mirerani, Biteko alisema ukuta uliojengwa hapo umeleta manufaa makubwa kwa Serikali na kwa jamii kwa ujumla sababu watu hawatoroshi madini tena na hivyo kupelekea ongezeko la mapato mpaka kufikia bilioni 2.1.
Aidha, Waziri Biteko, amebainisha kwamba, bei ya Madini ya Tanzanite imepanda katika soko la dunia, na hiyo inatokana na udhibiti mzuri uliowekwa na Serikali ya awamu ya Tano.
Amekiri kuwa kwa sasa watu hawatoroshi madini hivyo madini hayo yamekuwa bidhaa adimu katika soko la dunia hivyo kupelekea bei kupanda.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Profesa Simon Msanjila, amewataka wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite mkoani Manyara kufuata utaratibu na sheria zilizowekwa na Serikali, na pia kutoa taarifa sahihi  kwa Serikali.
Aidha, Profesa Masanjila, ameiagiza Tume ya Madini iongeze watumishi wa kutathimini madini ya Tanzanite ili kazi ziende kwa haraka na uhakika.

Comments