Skip to main content

Kufuatia ziara ya Naibu Waziri Nyongo soko la madini kufunguliwa Kahama

Kufuatia ziara ya Naibu Waziri Nyongo soko la madini kufunguliwa Kahama

Na Greyson Mwase, Kahama
Ofisi ya Afisa Madini Mkazi, Mkoa wa Kimadini wa Kahama inatarajia kuanzisha soko la madini mapema ikiwa ni moja ya mikakati ya Serikali kupitia Wizara ya Madini katika kudhibiti utoroshwaji wa madini.
Kutoka kulia Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo na Kamishna Msaidizi- Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini, Ali Said Ali wakisikiliza kero za wamiliki wa mitambo ya kuchenjulia dhahabu (hawapo pichani) kupitia mkutano maalum uliofanyika Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga.
Hatua hiyo imekuja kufuatia ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo aliyoifanya mapema leo tarehe 30 Machi, 2019 katika Wilaya ya Kahama lengo likiwa ni kukagua shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini ya dhahabu, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.
Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Nyongo aliambatana na Kamishna Msaidizi- Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini, Ali Said Ali wataalam kutoka Tume ya Madini pamoja na wawakilishi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Mara baada ya kufanya ziara katika baadhi  ya mitambo ya kuchenjua dhahabu, Nyongo alifanya kikao na wamiliki wa mitambo hiyo na kusikiliza kero mbalimbali pamoja na kuzitatua.
Mara baada ya kusikiliza kero husika ikiwa ni pamoja na ya kutokuwepo kwa soko la madini katika Wilaya ya Kahama, Naibu Waziri Nyongo alimwelekeza Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama,  Adrea Fabian kuhakikisha sehemu ya ofisi yake inatumika kama soko la madini ya dhahabu ambapo wauzaji na wanunuzi watakuwa wanafanya biashara huku serikali ikipata mapato yake, kauli ambayo ilipokelewa kwa shangwe na wafanyabiashara wa madini ya dhahabu.
Aliendelea kusema kuwa kutokuwepo kwa soko la madini katika Wilaya ya Kahama, kunachochea utoroshwaji wa madini ya dhahabu kwakuwa inakuwa vigumu kwa wauzaji wa madini hayo kusafiri umbali mrefu hadi Geita kwa ajili ya kwenda kuuza madini hayo.
“Hapa tunataka kuhakikisha biashara ya madini inafanyika hapa hapa ili kuwarahisishia wafanyabiashara wa madini ya dhahabu huku Serikali ikipata mapato yake,” alisisitiza Naibu Waziri Nyongo.
Katika hatua nyingine, Nyongo aliutaka uongozi wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama kushirikisha mamlaka nyingine za Serikali kama vile Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Mabenki na soko kuanza mara moja.
Aidha, Naibu Waziri Nyongo aliwataka wamiliki wa mitambo ya kuchenjua dhahabu kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli katika kulinda rasilimali za madini kwa kutoa ushirikiano kwa Wizara ya Madini.
Wakizungumza katika nyakati tofauti wamiliki wa mitambo ya kuchenjulia dhahabu walioshiriki katika kikao hicho mbali na kumpongeza Naibu Waziri Nyongo wamesema kuwa uwepo wa soko hilo utawarahisishia sana biashara ya madini kutokana na kuepukana na matapeli huku serikali ikipata mapato yake stahiki.
Walisema kabla ya uamuzi huo wamekuwa wakisafirisha madini hadi Geita kwa ajili ya kuuza hali inayopelekea baadhi yao kuuza kwa watu wasio waaminifu.

Comments