KAMATI YA BUNGE YATEMBELEA KITUO CHA NAIC ARUSHA


SERIKALI imewaagiza wataalam wa mifugo wa  halmashauri zote nchini kutoka ofisini na kwenda kutoa Elimu kwa wafugaji juu ya  utumiaji wa mbegu bora za ng'ombe  zinazozalishwa na kituo cha Taifa cha Uhimilishaji Mifugo kwa njia ya chupa NAIC kilichopo Arumeru, Mkoani Arusha.

Agizo hilo limetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Migugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel alipokuwa akitoa Taarifa  kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo, na Maji walipotembelea kituo hicho Jijini Arusha.
Prof. Gabriel, alisema kuwa ili kuendana na azma ya serikali ya  uchumi wa viwanda, ni lazima wafugaji nchini wabadilike na kuanza kufuga kwa tija kwa ajili ya kupata  nyama bora, maziwa, ngozi na Kwato, ambapo malighafi hizo zitakidhi mahitaji ya viwanda hapa nchini.
Aidha, Katibu Mkuu Mifugo ametoa agizo hilo kufuatia idadi ndogo ya wafugaji waliopewa elimu  mwaka 2017/2018  kuwa  hairidhishi hivyo kuna kila sababu ya watendaji wa halmashauri wanaohusika na idara ya mifugo kutoka ofisini na kwenda kutoa elimu kwa wafugaji ili wabadilike na kufuga kisasa.

Katibu Mkuu aliieleza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuwa kwa kipindi cha mwaka 2018/2019 ni wafugaji Elfu 58 pekee ndiyo waliopewa elimu ya uhimilishaji katika kituo cha NAIC ambacho ni cha kwanza katika Bara la Afrika kwa ubora, kikizalisha mbegu Elfu 60 kwa mwaka  ukilinganisha na mahitaji halisi ambayo ni Elfu 50 kwa mwaka.
"Idadi ya wafugaji waliopewa elimu ni ndogo na mwitikio wa utumiaji wa mbegu hizi hauridhishi, wakati kituo kinazalisha mbegu za kutosha kwa mahitaji ya wafugaji wote nchini, hivyo nawaagiza wataalamu wote watoke ofisini waende kwa wafugaji kutoa elimu juu ya utumiaji wa mbegu hizi." Alisema Prof. Gabriel.
Pia, Prof. Gabriel alitumia fursa hiyo kuwataka  wafugaji wote nchini  kuondokana na dhana potofu kuwa mbegu za chupa zinaharibu kizazi cha Ng'ombe, jambo ambalo sio sahihi na kuwataka kutumia mbegu hizo ili kuondokana na ufugaji wa mifugo mingi ambayo haina tija.
Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega, amesema hali ya usambazaji wa mbegu hizo kwenye vituo vilivyopo kanda saba nchini hairidhishi kutokana na baadhi ya waataalamu kutotimiza wajibu wao wa utoaji elimu kwa wafugaji.
"Serikali inauza mbegu hizi kwa ruzuku ili wafugaji wasiokuwa na uwezo waweze kumudu gharama ya Shilingi Tano kwa dozi ya mbegu moja, lakini kuna baadhi ya wataalamu wananunua mbegu hizi na kuziuza kwa bei kubwa kati ya Shilingi Elfu 15 na Elfu 40 huku halmashauri zikifumbia macho hali hiyo inayosababisha mbegu kutonunuliwa kwa wingi." Alisema Naibu Waziri Ulega.
Aidha aliwataka wafanyabishara binafsi wanaoagiza  mbegu hizo za  chupa kutoka  nje ya nchi na kuwauzia wafugaji kwa bei ya  Shilingi 50 hadi Laki Moja waache mara moja, badala yake  wanunue mbegu kutoka NAIC kwa sababu mbegu hizo ni bora.
"Serikali katika bajeti yake ya mwaka 2017/2018 ilitenga fedha kwa ajili ya kununua madume bora 28 kutoka nchi za nje, lengo likiwa ni kuwezesha wafugaji kupata mbegu bora na kisasa, hivyo hakuna sababu ya kununua mbegu kutoka nje ya nchi."Alisema.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo, na Maji Mhe. Mahamoud Mgimwa, amesema utumiaji wa mbegu hizo utawezesha wafugaji kufuga kwa tija na kupata soko la uhakika la bidhaa za mifugo ndani na nje ya Nchi.
"Kikubwa hapa wafugaji wabadilike kutoka kwenye ufugaji wa mazoea na kufuga kisasa kwa kutumia mbegu hizi za NAIC ili tushiriki uzalishaji wa malighafi za viwanda vyetu vinavyoanzishwa kwa wingi hapa nchini."Alisema.
Mwisho.
Imetolewa: Kitengo cha Mawasiliano
   Wizara ya Mifugo na Uvuvi
   21.03.2019

Comments