Mambo ya msingi ya kuzingatia ili kufanya biashara yenye faida
Get link
Facebook
X
Pinterest
Email
Other Apps
Moja ya changamoto kubwa ambayo watu wengi wanakutana nayo ni kushindwa
kujua biashara gani wafanye kwenye maeneo yao ili kuweza kupata faida.
Mara nyingi watu wamekuwa wakiomba ushauri sehemu mbalimbali ikiwemo
kwenye mitandao kuhusu biashara gani wafanye kwenye maeneo yao.
Ili kuweza kutengeneza biashara yenye faida katika eneo unaloishi au
unalopendelea kufanya biashara yako nakushauri ufanye mambo haya matano.
1. Fanya utafiti mdogo wa kujua biashara gani inayofaa kwa eneo hilo.
Ni muhimu sana kufanya utafiti mfupi ili kujua kama wazo lako la
biashara linaweza kufanikiwa kwa eneo unalotaka kufanyia biashara. Sio
kila wazo la biashara linaweza kutengeneza biashara kubwa na yenye
faida.
2. Kuwa tofauti, kuwa mbunifu.
Kama kuna soko la biashara unayotaka kufanya ni dhahiri kwamba kuna watu
wengine wanafanya biashara hiyo. Jiulize ni jinsi gani unaweza
kujitofautisha na watu hao? Kama huna njia ya kujitofautisha nakushauri
tu uachane na hiyo biashara maana utaumiza sana kichwa. Hakuna kitu
kinachoumiza kichwa kwenye biashara kama ushindani usiokuwa na tofauti,
kama kuna mwenye mtaji mkubwa kushinda wewe atakuondoa sokoni. Mara zote
jua ni mbinu gani za kibunifu na za utofauti za kukuwezesha kukuza
biashara yako.
3. Kua kwanza wewe ndio biashara yako ikue.
Inashangaza ni kiasi gani watu wanataka biashara zao zikue wakati wao
wenyewe hawakui. Jua siri hii moja ”Lazima wewe ukue kwanza ndipo
biashara yako nayo ikue”. Ili wewe kukua unahitaji kujifunza kila siku
kuhusiana na biashara unayofanya na biashara nyingine kwa ujumla.
Tunaishi kwenye zama ambazo kujifunza kuko kwenye ncha za vidole,
mtandao una kila kitu unachotaka kujifunza. Tembelea mitandao ya
kujifunza na utapata mbinu bora ka kukuza biashara yako. Usitegemee
kufanikiwa kwa kufanya biashara kwa mazoea, kujifunza ni muhimu sana.
4. Kuwa na usimamizi wa kutosha kwenye biashara yako.
Watu hawaaminiki kwenye fedha, ni tatizo sana kama umejinyima na kupata
mtaji wa biashara halafu unaianzisha na kuwapa watu wengine waisimamie.
Ni rahisi sana kushindwa au kupata hasara kwa njia hii. Ni vigumu sana
kupata mtu anayeweza kuwa na uchungu na biashara yako. Nakushauri kama
huna muda wa kufuatilia biashara yako kwa karibu ni heri utumie hiyo
fedha yako kufanya mambo mengine yatakayokuingizia fedha kidogo kuliko
kwenda kuipoteza huku ukiona.
5. Kuwa na uvumilivu.
Kama kila ukianzisha biashara na kuona hailipi unaacha na kuanzisha
nyingine, utafanya kila aina ya biashara na hutaona mafanikio yoyote.
Bishara sio rahisi kama watu wanavyoamini, biashara inahitaji uvumilivu
na ustahimilivu. Ni vigumu na mara chache sana mtu anaweza kuanzisha
biashara na akaenda vizuri bila ya kupata misukosuko. Kwenye biashara
halisi kuna misukosuko mingi sana, unaweka mkakati mzuri na kujua faida
itapatikana ila vinatokea vikwazo na kukurudisha nyuma. Katika nyakati
hizi ndio unatakiwa kujifunza na kama ukivuka nyakati ngumu unakuwa
umeongeza kinga kwenye biashara yako. Unapojifunza utajua ni wapi
ulipokosea hivyo kuepuka kurudia makosa.
6. Usiitegemee biashara mwanzoni.
Kama nilivyosema hapo juu biashara inachukua mwaka mmoja na wakati
mwingine miaka miwili kuweza kusimama na kujiendesha yenyewe na
kutengeneza faida. Kipindi cha mwanzo cha biashara ni kigumu sana na
hutakiwi kuondoa fedha yoyote kwenye biashara kwa matumizi yasiyo ya
biashara. Usianzishe biashara na wakati huo huo ukaanza kuitegemea kwa
kuishi, biashara hiyo itakufa.
Biashara ni nzuri sana kama umejipanga na unajua ni nini unafanya. Ila
kama hujajipanga au umeiga, biashara inaweza kuwa ngumu sana kwako kiasi
cha kuachana nayo kabisa. Kwa ushauri huu nafikiri unaweza kubadili
mtazamo wako na mbinu za kufanya biashara.
Comments
Post a Comment