Dawa za vitamini A kupewa kipaumbele

Mkuu wa Idara ya Kilimo, Ushirika na Umwagiliaji Joseph Machibya kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Lishe Wilaya ya Bukombe amemuagiza Mganga Mkuu wa Wilaya kuhakikisha anaweka kipaumbele ununuzi wa dawa hasa za  vitamin A kwa ajili ya kuboresha afya za watoto chini ya umri wa miaka mitano katika ukuaji wao.
Wito huo  ameutoa katika kikao cha mapitio  ya shughuli za lishe kwa kipindi cha Julai – Disemba 2018 katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauli tarehe 5 Februari, 2019.
Pia Machibya amemuagiza Afisa Lishe Wilaya kuhakikisha anawashirikisha wadau wote katika uandaaji wa bajeti 2019/2020  ili Halmashauri iwe na mpango mkakati mmoja utakao leta tija katika suala la lishe bora.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe Julai –Disemba 2018 Afisa Lishe Wilaya Ladislaus Willium Magaso alisema hadi kufikia Disemba 2018 IMA world Heaith ilitoa Tsh. 57,601,000/= kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za lishe ambazo ni ufuatiliaji wa matumizi ya chumvi yenye madini joto, ukaguzi wa wafanyabiashara wa chumvi, kutembelea kaya zenye watoto chini ya umri wa miaka mitano ili kutoa elimu ya lishe bora, kufanya mikutano kwa wasimamizi wa wahudumu wa afya ngazi ya kijiji, kufanya mikutano ya  kamati ya uendeshaji wa shughuli za lishe ngazi ya Wilaya, uhamasishaji juu ya ulishaji sahihi wa watoto, kuwezesha wajumbe wa kamati ya Afya ya Wilaya kukusanya takwimu na ufuatiliaji wa zoezi la utoaji wa Vitamini A na dawa za Minyoo.
Kwa upande wake Katibu wa Afya Wilaya ya Bukombe Zacharia Isack alisema hapo nyuma kulikuwa na changamoto ya uchangiaji wa huduma za afya uliopelekea mapato ya huduma za afya kushuka, baada kuanzishwa kwa mfuko wa afya ya jamii (CHF iliyoboreshwa) tunategemea kuwepo kwa ongezeka kubwa la mapato ya ndani yatakayopelekea kuboresha maisha ya akinamama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano kwa asilimia kubwa.

Mkuu wa Idara ya Kilimo, Ushirika na Umwagiliaji Joseph Machibya akifungua kikao kwa niaba Mwenyekiti wa Kamati ya Lishe Wilaya ya Bukombe

Afisa Lishe Wilaya Ladislaus Willium Magaso akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe
Mwekahazina wa Wilaya ya Bukombe John Bernard Majubu akichangia mada wakati wa kikao

Baadhi ya wajumbe wa kamati ya lishe Wilaya

Comments