WAZIRI APIGA MARUFUKU HALMASHAURI KUTUMIA WAKANDARASI


Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Faustine Ndugulile amewaagiza watendaji wa halmashauri zote nchini kutotumia wakandarasi kujenga miradi mbalimbali inayohusu sekta ya afya.

Ametoa agizo hilo mkoani Ruvuma wakati alipotembelea na kujionea ukarabati na ujenzi wa Chuo cha Wauguzi Songea na Chuo cha Maendeleo ya Jamii Mlale katika ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Amesema kuwa miradi hiyo inatakiwa kutumia mtindo wa 'Force Account', ambao unatumia mafundi wa kawaida kujenga miradi hiyo.

"Fedha zote za maendeleo Ndani ya Wizara yetu ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, utaratibu utakuwa ni 'Force Account'. Kibali cha kwenda kwa wakandarasi kitatoka kwa mawaziri, kwasababu mwisho wa siku ninayewajibika ni mimi", amesema Dkt. Faustine Ndugulile.

Naibu Waziri Ndugulile amefikia hatua hiyo baada ya kupokea taarifa ya kuanza kwa mchakato wa ujenzi wa baadhi ya majengo na ukuta wa Chuo cha Waganga mkoani humo, ambao ungegharimu zaidi ya shilingi milioni 900, akisema kwamba endapo ungetumika mfumo wa 'Force Account' zingejenga jengo hilo na ukuta.
Chanzo:Eatv

Comments