WALIOHUSIKA NA UJAMBAZI BUKOMBE WATAKAMATWA

Mbunge wa Jimbo la Bukombe na Naibu Waziri wa Madini, Doto Mashaka Biteko amewahakikishia wananchi wa Kijiji cha Lyobahika , Kata ya Uyovu Wilayani Bukombe kuwa wote waliohusika na tukio la ujambazi lililotokea hapo Aprili 11, 2018 na kusababisha uharibifu mkubwa wa nyumba  watakamatwa.
Biteko alibainisha hayo Aprili 12, 2018 alipofika kutoa pole kwa wananchi wa eneo kulikotokea tukio la ujambazi lililosababisha uharibifu mkubwa wa Mali za Emanuel Samwel Sayi maarufu Ndokeji na kuporwa kiasi cha Shilingi Milioni Arobaini  na vifaa vingine ikiweno simu za mkononi.

Akizungumzia tukio hilo, Mtendaji wa Kata Bartazari  alisema tukio hilo lilitokea majira ya Saa Sita  na Nusu usiku ambapo watu wasiofahamika walivamia eneo hilo wakiwa na silaha za moto ambapo walichoronga na kuweka kitu chenye mlipuko na kubomoa ukuta wa nyuma wa duka hilo na kufanikiwa kupora.
Biteko aliwahakikishia wananchi hao kuwa Serikali inafuatilia suala hilo kwani ni jukumu lake kuhakikisha usalama kwa wananchi wake. 

Alimuagiza Mkuu wa Kituo cha Polisi Runzewe kuhakikisha uchunguzi unakamilika mapema ili kuwabaini wahusika wote wa tukio hilo.
"Serikali itahakikisha wale wote waliouhusika na tukio hili wanakamatwa na sheria inachukua mkondo wake,"alisisitiza Biteko.

Aidha Biteko alisema taarifa alizopata ni kwamba matukio ya uhalifu yameongezeka Jimboni humo na aliiagiza Kamati ya Ulinzi na Usalama kuhakikisha upelelezi unafanyika ili kukomesha matukio mbalimbali ya kihalifu.

Aliwataka  wananchi jimboni humo kuendeleza ulinzi shirikishi na kuwabaini na kuwataja wananchi wanaotishia  usalama kwenye maeneo mbalimbali.
"Haya matukio kuna wananchi hapa lazima wanahusika ambao wanatoa taarifa kwa wahalifu kuhusiana na hali ya hapa. Wananchi msiogope kuwataja mnaowashakia ili hatua zichukuliwe," alisema.

Mbunge na Naibu Waziri huyo alifika  Jimboni humo kwa ajili ya kutoa pole kwa wahanga hao ikiwemo wazazi wake ambao pia walivamiwa nyumbani kwao Kijiji cha Imuhozyo Kata ya Bulangwa.

Comments