Sierra Leone Yafanya Uchaguzi Wa Marudio.

Wapiga kura nchini Sierra Leone wamejitokeza katika vituo vya kupigia kura hii leo kumchagua rais mpya katika kinyang’aniro kikali cha duru ya pili ya uchaguzi kati ya kiongozi wa upinzani Julius Maada Bio na mgombea wa chama tawala Samura Kamara.
Bio, wa chama cha upinzani cha Sierra Leone People’s Party – SLPP, alipata ushindi mwembamba katika duru ya kwanza ya uchaguzi mnamo Machi 7 akiwa na asilimia 43.3. Mpinzani wake Kamara alipata asilimia 42.7. Duru ya pili iliitishwa kwa sababu hakuna mgombea aliyepata asilimia 55 ya kura inayohitajika ili kutangazwa kuwa mshindi wa moja kwa moja.
Kamara, mwenye umri wa miaka 67, mbombea wa chama tawala cha All People’s Congress – APC, anaahidi kuufufua uchumi, wakati Bio akiahidi kuumaliza ufisadi na kutoa elimu ya bila malipo. Takribani Wasierra Leone milioni 3.18 wamesajiliwa kupiga kura. Rais Ernest Bai Koroma anaondoka madarakani baada ya kuongoza kwa mihula miwili ya miaka mitano kila mmoja.

Comments