Ethiopia: Zaidi Ya Watu 1,100 WamekamatwaTangu Hali Ya Dharura Ilipotangazwa.

Zaidi ya watu 1,100 wameripotiwa kukamatwa tangu nchi ya Ethiopia ilipotangaza hali ya dharura kufuatia kujiuzulu kwa Waziri Mkuu wake mwezi uliopita. Redio Fana yenye uhusiano na redio ya taifa ilisema watu 1,107 wamekamatwa kwa kukiuka amri ya dharura, ambayo inasitisha kwa muda katiba na kuwaruhusu polisi kuwashikilia watu bila kuwafungulia mashtaka.
Fana iliripoti ikimnukuu Tadesse Hordofa, mwenyekiti wa bodi inayoangalia amri hiyo kwamba watu hao walikamatwa kwa kuwauwa raia wasio na hatia na vikosi vya usalama, kuchoma moto nyumba na taasisi za kifedha, kuharibu majengo ya serikali na taasisi za umma pamoja na kufunga barabara.
Hatua isiyotegemewa ya kujiuzulu Hailemariam Desalegn ilikuja baada ya zaidi ya miaka miwili ya maandamano ya kuipinga serikali na kuongezeka mgawanyiko katika chama tawala nchini humo.
Chama cha Ethiopian People’s Revolutionary Democratic Front-EPRDF kwa mara ya kwanza kimemteuwa kiongozi wake kutoka kabila la Oromo, Abiy Ahmed. Kiongozi huyo anatarajiwa kuapishwa kama Waziri Mkuu mpya mwanzoni mwa wiki ijayo

Comments