Zaidi Ya Vijana 900 Wapewa Elimu Ya Ujasiriamli.


Taasisi ya Ujasiriamali na Ushindani Tanzania (TECC), kupitia kampeni ya kijana jiajiri, imetoa mafunzo ya ujasiriamali kwa zaidi ya vijana 930, yanayofadhiliwa na Mradi wa Tanzania LNG Plant
Abdul Juma Meneja Uwezeshaji na Uhamasishaji wa Ujasiriamali kutoka TECC, wakati akifungua mafunzo ya vijana 70 wa Wilaya ya lindi yaliyofanyika Manispaa ya Lindi mkoani humo, amesema tangu kampeni hiyo ya kijana jiajiri ilipoanzishwa mwaka 2015 kati ya vijana hao 930 waliopatiwa mafunzo vijana 260 wameanzisha biashara zao wenyewe.

“Kabla ya hapo vijana wengi hawakuwa na elimu ya ujasiriamali lakini sasa tumeanza kuona biashara walizoanzisha na wanazozifanya baada ya mafunzo kwa kushirikiana na Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO), na Mfuko wa Rais wa Kujitegemea ambao ndiyo wanawawezesha vijana kuwapa mikopo baada ya kupatiwa mafunzo hayo,” amesema Juma.

Pamoja na mambo mengine, Juma amesema mafunzo hayo yana lengo la kuwajengea vijana uwezo wa kuzitumia fursa zinazowazunguka na kutumia fursa hizo kwa kuchanganya na juhudi zao binafsi kwa kuanzisha miradi ya biashara ambayo itakuwa endelevu na kuwa na uwezo wa kujiajiri wenyewe pamoja na kuwaajiri vijana wengine.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Herieth Kaluwa amewataka washiriki hao wa mafunzo ya ujasiliamali kuzingatia muda na matumizi bora ya fedha katika biashara zao huku akiiomba taasisi ya TECC kupanua wigo wa kuwafikia vijana wengi zaidi hasa wa vijijini.
“Muda na kuzingatia nidhamu ya matumizi ya fedha ni jambo muhimu katika kufanya biashara kama hukuweza kuyazingatia haya unaweza ukasema biashara ngumu au ukitumia fedha ya biashara bila kuwa na nidhamu nayo unaweza ukafilisika kwa kuyumba kwa mtaji,” amesema Kaluwa.

Comments