SERIKALI: MAAFISA HABARI NA MAWASILIANO TUMIENI TOVUTI KUTANGAZA SHUGHULI ZA MAENDELEO YA WANANCHI

Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Rodney Thadeus akizungumza na Maafisa Habari na Mawasiliano Serikali wakati wa mafunzo kuhusu mwongozo wa uandishi wa tovuti za Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa yaliyofungwa leo Ijumaa Machi 23, 2018 Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yaliandaliwa na Mradi wa Uimarishaji Mifumo ya Sekta ya Umma (PS3) kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kupitia ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID).
Baadhi ya Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini wakifuatiliano mafunzo mafunzo kuhusu mwongozo wa uandishi wa tovuti za Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa yaliyofungwa leo Ijumaa Machi 23, 2018 Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yaliandaliwa na Mradi wa Uimarishaji Mifumo ya Sekta ya Umma (PS3) kupitia ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID).
Afisa Habari kutoka Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Atley Kuni akizungumza na Maafisa Habari na Mawasiliano Serikali wakati wa mafunzo kuhusu mwongozo wa uandishi wa tovuti za Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa yaliyofungwa leo Ijumaa Machi 23, 2018 Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yaliandaliwa na Mradi wa Uimarishaji Mifumo ya Sekta ya Umma (PS3) kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kupitia ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID).

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

MAAFISA Habari na Mawasiliano katika Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini, wametakiwa kuongeza kasi ya matumizi ya  mitandao ya kijamii ikiwemo tovuti  ili kuleta mageuzi yaliyokusudiwa na Serikali katika kutangaza shughuli za maendeleo ya wananchi.

Hayo yamesemwa leo (Ijumaa Machi 23, 2018) Mkoani Morogoro na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Rodney Thadeus wakati wa kufunga mafunzo ya siku nne kwa Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini yaliyohusu mwongozo wa uendeshaji wa  Tovuti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini yaliyoandaliwa na Mradi wa Uimarishaji Mifumo ya Sekta za Umma (PS3) kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kupitia Ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID).

Thadeus alisema Serikali kupitia Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Wakala ya Serikali Mtandao (EGA) na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Mradi wa Uimarishaji Mifumo ya Sekta ya Umma (PS3) kwa pamoja waliandaa mwongozo huo ili kuhakikisha kuwa tovuti za Mikoa na Halmashauri zinakuwa nyenzo muhimu ya taarifa za Serikali.

“Mafunzo mliyoyapata ni vyema mkahakikishe kuwa tovuti zenu zinaweza kusaidia maendeleo ya wananchi kwa kutangaza shughuli za maendeleo pamoja na kuzingatia thamani ya fedha zilizotolewa na wadau wetu wa maendeleo kwa kuleta mabadiliko ya mwonekano wa tovuti zetu” alisema Thadeus.

Aidha alisema kupitia mafunzo yaliyotolewa kuhusu mwongozo huo, ni matarajio ya Serikali kuwa tovuti zote za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa zitakuwa zimesheni habari zilizoandikwa kwa usahihi pamoja na kuwekwa taarifa za mara kwa mara hatua itayowezesha wananchi wengi Zaidi kuweza kuzitembelea na kupata huduma zinazostahili.

Alisema Ofisi yake ipo tayari kufanyia kazi na Maafisa Habari na Mawasilino waliopo katika Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa iwapo kutajitokeza changamoto yoyote inayohusu usimamizi, uendeshaji na uboreshaji wa maudhui ikiwemo mafunzo ya mara kwa mara kwa watendaji wa tovuti hizo.

Thadeus alisema Idara ya Habari (MAELEZO) itahakikisha kuwa inafanya mawasiliano ya mara kwa mara na Watendaji Wakuu wa Mikoa na Halmashauri za Wilaya ili kuhakikisha kuwa Maafisa Habari na Mawasiliano ambao ndio watendaji  wa tovuti hizo wanapata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Wakuu mbalimbali wa Idara na Vitengo katika Mikoa na Halmashauri zote nchini.

Kwa upande wake, Afisa Habari kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Atley Kuni alisema malengo ya Serikali ni kuhakikisha kuwa tovuti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa zinakuwa kiunganishi baina ya Serikali na wananchi kwa kuhakikisha zinatangaza taarifa mbalimbali za mafanikio ya Serikali katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Tumepanga tuwe na jarida maalum litakalokuwa na habari mbalimbali za mafanikio ya miradi ya maendeleo, ambazo zitakuwa zikiandikwa na Maafisa Habari na Mawasiliano waliopo katika Mikoa na Halmashauri ambazo zitakuwa zikiakisi maendeleo yaliyoweza kupatikana mara baada ya kuanzishwa kwa tovuti hizi” alisema Kuni.

Aidha aliongeza kuwa Maafisa Habari na Mawasiliano wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa hawana budi kuongeza ubunifu ili kuhakikisha kuwa tovuti hizo pia zinaweza kuwa chanzo kikuu cha mapato katikas maeneo yao ya kazi.

MWISHO

Comments