JOKATE KIDOTI MAPYA YAIBUKA BAADA YA KUTUMBULIWA,WEMA ATAJWA

Aliyekuwa Kaimu Katibu wa Idara ya Uhamasishaji na Chipukizi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UV-CCM), Jokate Mwegelo ‘Kidoti’BAADA ya wikiendi iliyopita aliyekuwa Kaimu Katibu wa Idara ya Uhamasishaji na Chipukizi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UV-CCM), Jokate Mwegelo ‘Kidoti’ kutumbuliwa katika nafasi hiyo, staa wa filamu za Kibongo, Wema Isaac Sepetu ametajwa, Risasi Mchanganyiko linakupa habari kamili.Mara tu baada ya sakata hilo kuchukua nafasi kwenye vyombo vya habari na mitandao mbalimbali ya kijamii, habari za ndani zinaeleza kwamba, Wema alianza kutajwa katika kumrithi mwanadada Jokate kwenye kiti hicho.

Chanzo cha ndani ya umoja huo wa vijana kililieleza Risasi Mchanganyiko kuwa, nafasi aliyoondolewa Jokate kuna uwezekano mkubwa wa kushikiliwa na Wema na ndiyo maana siku za hivi karibuni ameonekana kuwa mwenye furaha tofauti na alivyokuwa siku za nyuma.
“Nafasi ya Jokate itachukuliwa na Wema na Jokate atapewa nafasi ya juu zaidi ila kwa sasa ni siri kubwa hata ukiwauliza viongozi hawataweza kukueleza kuhusu hilo,” kilidai chanzo.

MSIKIE KIONGOZI UVCCM
Akizungumza na Risasi Mchanganyiko, Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka alisema kuwa, uamuzi wa kumuondoa Jokate ni wa kawaida na ni wa kamati ya utekelezaji ya UV-CCM na ndicho chombo ambacho kina dhamana ya kuweka na kuondoa na mara zote anapoondoka mtu au anapoletwa mtu, kamati huwa inajiridhisha na ina sababu zake hivyo hayo ni masuala ya kiutawala na kiuendeshaji na yanabakia kwenye uendeshaji wa vikao.

Wema Isaac Sepetu
Bahati nzuri Jokate alikuwa anakaimu, hakuwa amethibitishwa kwa mujibu wa taratibu zetu ndani ya jumuiya, ndani ya jumuiya ili uweze kuwa kamili ni lazima uthibitishwe na Baraza Kuu la UV-CCM, sasa yeye kwa kipindi chote cha mwaka mmoja hakuwa amethibitishwa kwa sababu alikuwa anakaimu tu.
“Kwa hiyo yapo mambo pengine si mabaya si mema au mema kabisa hayo yote hata kama yapo hatuwezi kuyatoa nje ya kikao chetu, huo ni utaratibu wa kawaida, Jokate hajakosea chochote, bali ni mambo ya kupokezana vijiti tu na hakuna mtu ambaye tumepanga aje achukue nafasi kama wengi wanavyodai kwa sababu yote hayo ni utaratibu wa vikao,” alisema kiongozi huyo.

Aliendelea kueleza kuwa, baada ya vikao vitakapokaa, kama jambo hilo liko kwenye ajenda litajadiliwa na atawekwa mtu, lakini kama halipo halitajadiliwa.
Alipoulizwa kuhusu Wema kudaiwa kuwa ndiye atakayeirithi nafasi hiyo, Shaka alisema kuwa, hayo hayafahamu kwa sasa ndiyo anayasikia na kuhusu Jokate kupewa nafasi ya juu zaidi pia hana taarifa hizo.
Risasi Mchanganyiko lilifanya jitihada za kumtafuta Jokate ili kumsikia ana lipi la kusema juu ya kutumbuliwa katika nafasi hiyo, lakini simu yake ya mkononi iliita bila kupokelewa na hata alipotumiwa meseji kwa njia ya WhatsApp hakujibu chochote.
Jokate ambaye ni Miss Tanzania namba mbili aliteuliwa kushika nafasi hiyo Aprili, mwaka 2017 ambapo ameshikilia kwa mwaka mmoja hadi alipotumbuliwa Jumapili iliyopita baada ya kamati ya utekelezaji ya umoja huo chini ya mwenyekiti wake, Kheri James kukaa kikao cha siku moja kilichofanyika Dodoma na kufikia uamuzi huo

Comments