Maofisa CDA wapangiwa kazi nyingine Ni Baada ya Rais Magufuli Kuivunja

Wafanyakazi 260 wa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji wa Mji wa Dodoma (CDA) wamepangiwa vituo vipya vya kazi.

Kwa mujibu wa Waziri Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene wafanyakazi 150 kutoka kundi hilo wanabaki Manispaa ya Dodoma huku wengine 66 wakipelekwa katika halmashuri na mikoa mbalimbali nchini.

Amesema wafanyakazi 16 wamepelekwa Tamisemi, DART (14), Hospitali ya Benjamini Mkapa Dodoma (4), Chuo Kikuu cha Dodoma (3), Ofisi ya Waziri Mkuu (3), Wizara ya Ardhi (2) Ofisi ya Bunge (1) na Utumishi wa Umma (1).

Waziri Simbachawene amewataka wafanyakazi hao kuripoti katika vituo vyao vya kazi mara baada ya kupata barua na Serikali haitasita kufuta ajira ya mtumishi yeyote ambaye atakaidi agizo hilo.

Rais wa John Magufuli aliivunja rasmi CDA Mei mwaka huu  na kuagiza mali na shughuli zote zilizokuwa zikifanywa na CDA zihamishiwe Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.

Rais Magufuli alisema ameamua kuivunja CDA na kuhamishia majukumu yake katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ili kuondoa mkanganyiko wa utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisema mkanganyiko huo ulikuwa ukisababishwa na mgongano kati ya vyombo hivyo viwili.

Aidha, alisema mahitaji ya sasa yamedhihirisha kuwa hakuna haja ya kuwepo kwa CDA.

“Wananchi wa Dodoma wamelalamikia tatizo hili kwa muda mrefu, hata nilipokuwa kwenye kampeni zangu za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 walilalamika sana, sasa nimetekeleza niliyowaahidi,” alisema Dk Magufuli.
 
“Naamini kwa uamuzi huu malalamiko ya wananchi yatapata utatuzi na pia tutakuwa tumeondoa kikwazo cha umiliki wa muda mfupi wa ardhi uliosababisha wawekezaji kushindwa kujenga viwanda Dodoma.

CDA ilianzishwa kwa Amri ya Rais ya Aprili Mosi, 1973 na kutangazwa kupitia tangazo la Serikali namba 230.

Comments