MTANZANIA NA MZAMBIA WANASWA INDIA NA MZIGO WA "UNGA" KILO NNE


Kushoto ni Mtanzania aliyejulikana kwa jina la Pamela David Kirrita (41) akiwa na mwanamke mwingine raia wa Zambia Thelma Mkandawire (38) wakiwa mbaroni kwa tuhuma za kukutwa na kilo 4 za madawa ya kulevya aina ya cocaine katika hoteli moja kusini mwa jiji la New Delhi, India. 
Naibu Mkurugenzi Mkuu wa kikosi cha kupambana na madawa ya kulevya cha New Delhi (NCB) Rajinder Pal Singh amesema watuhumiwa walikamatwa katika hoteli iliyopo eneo la Mahipalpur jana Februari 4, 2017. 
“Baada ya kupata taarifa kutoka vyanzo vyetu, timu yetu ikatega mtego kwa Mkandawire aliyewasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Indira Ghandi akitokea ughaibuni akiwa na mzigo huo. 
“Baada ya kuchekiwa uwanjani pale aliondoka na taxi hadi hotelini. Timu yetu ilimfuatilia na kumuona mara alipofika hotelini akakutana na Pamela David Kirrita aliyekuwa aupokee huo mzigo”, alisema Mkurugenzi wa NCB tawi la New Delhi. 

Amesema walipohojiwa Kirrita alibainisha kuwa alikuwa akiishi katika hoteli moja katika kitongoji kiitwacho Vasant Kunj tokea Januari, na kwamba alikuwa na mawasiliano na mtu mwingine raia wa kigeni ambaye ndiye angempasia mzigo baada ya kuuchukua toka kwa Mkandawire. 

Polisi wanasema mzigo ulifichwa kwenye uwazi wa begi la safari, na kwamba Mkabdawire aliwahi kukamatwa nchini Pakistani mwaka 2015 na kukaa mahabusu kwa zaidi ya miezi sita, huku Pamela akikiri kutembelea India zaidi ya mara sita tokea mwaka 2006.

Kwa sheria za India, mshtakiwa atayekutwa na hatia ya madawa ya kulevya yaliyokuwa ya kibiashara ni kifungo cha kati ya miaka 10 ama 20 gerezani na faini ya Rs 1 lakh (sawa na dola za Kimarekani 15,000) ama Rs 2 lakhs (dola 3000).

Comments