Leo Tarehe 5/10/2016 ni Siku ya MWALIMU DUNIANI.



 

OKTOBA 5, SIKU YA MWALIMU DUNIANI
Na, Doto Biteko


Leo tarehe 5/10/2016 ni siku ya MWALIMU DUNIANI.

 Katika nchi nyingi duniani ni siku ambayo pia watu hutambua kazi za waalimu na hutumika kuwapa heshima kwa kutambua mchango wa MWALIMU katika Jamii. kila nchi huwa na namna yake ya kuadhimisha siku hii muhimu mfano katika nchi ya Afghanistan siku hii shule zote hufungwa na walimu na wanafunzi pamoja hukusanyika kwenye shule husika huaandaliwa chakula cha asili, muziki wa asili na burudani mbalimbali kwa ajili ya walimu na badaye zawadi mbalimbali hutolewa kwa walimu.

Kwa kifupi huwa ni siku ya furaha sana kwa walimu maana huinua hali ya kufanya kazi na huwavuta watoto wengi kuipenda kazi ya ualimu.

Siku ya leo imenipa tafakari sana, nimekumbuka nilipoanza Safari ya kuuelekea ualimu pale chuo cha ualimu Katoke ilikuwa safari iliyojaa furaha na matumaini mengi nakumbuka nilipofika getini kulikuwa na walinzi (wanachuo) wakanikaribisha karibu sana Mwalimu nilianza kujiuliza hivi tayari nimekua mwalimu? Furaha yangu ilizidi sana. Baada ya kumaliza masomo ya ualimu niliajiriwa kama mwalimu daraja la IIIA katika shule ya msingi Nyang’hanga, niliianza kazi hiyo kwa mapenzi yangu yote!

Niliipenda kazi yangu, niliyapenda mazingira pamoja na kwamba ilikua kijijini sana(pengine kwasababu pia nilizaliwa na kukulia kijijini sana) niliwapenda sana wanafunzi wangu. Nilijiona mwenye bahati kuheshimika kama mzazi katika umri ule mdogo wa miaka23, jamii walinipenda na wanafunzi wangu walinipenda sana.

Niliposhika zamu yangu ya wiki wanafuzi na hata wazazi wao walijua ni zamu yangu maana walijua nilisimamia kila kitu mwenyewe kuanzia Kuhesabisha namba, kukimbiza watoto mchakamchaka,kusimamia kufanya usafi wa mazingira,gwaride la asubuhi utulivu madarasani na hata kazi za Elimu ya kujitegemea(E/K) nk.ukweli viranja nao walibidi kufanya kazi kwa bidii zaidi.Naikumbuka sana kazi ya ualimu

Ndiyo! Leo ni siku yetu walimu, katika kusherehekea siku hii, leo nimeiazimisha siku hii na walimu wa Tarafa ya Siloka katika wilaya ya Bukombe katika kusherehekea siku hii. Nimekumbuka mengi sana, nimeona walimu walivyosherehekea siku yao kwa furaha kuu. Pamoja na mambo mengine nimewasikia wakidokeza kutokuthaminiwa na jamii!Hapanikajifunza kitu Mbona hawathaminiwi?

Kazi ya ualimu ni kazi ya uumbaji, ni kazi inayoanzisha maisha ya mwanadamu kwenye ustaarabu wa dunia, hii ndiyo kazi iliyofanywa na mitume wa mwanzo kabisa katika ulimwengu. Wote waliofanya kazi ya Ualimu wameacha alama ya kudumu katika ulimwengu Huu. Akina Plato, Socrates, Aristotle, Alexander The Great, Yesu Kristo, Mtume Muhamad na hata zama za akina Mahtma Gadhi hadi wa kati Julius Nyerere. Wote hawa wanakumbukwa kwa kuacha alama kwenye maisha ya ulimwengu na bila Shaka kwakuwa wote hawa walikua walimu.

Tunaposherehekea siku hii walimu tutambue kazi yetu hii ni kiini cha Taaluma nyingine, tusikubali mtu awaye yote akadunisha taaluma ama akatuona dhalili au tusio muhimu. Nafahamu zipo changamoto nyingi zinazotukabili walimu ikiwemo madeni mbalimbali yanatokanayo na mishahara na yale yasiyokua ya mishahara, nafahamu mishahara ilipwayo kwa walimu bado ni midogo sana ukilinganisha na gharama halisi za maisha. Hata hivyo ni vema tukatambua hakuna mtu atakaye kuja kupigania hadhi yetu isipokua kuwa sisi wenyewe walimu.

Jamii nayo kwa upande mwingine inatulaumu kutokana na vitendo vya wachache wetu, ikiwemo ulevi, rushwa na hata kuwa na mahausiano ya mapenzi na wanafunzi mambo haya yanapotendeka yanatupunguzia hadhi kwa jamii. Ni wajibu wetu sote kuonyana na kushauriana kuwa pamoja na maisha binafsi tumebeba chapa ualimu wetu ambao ni taaluma yetu sote.

Walimu tunaposherehekea siku hii ya leo tutambue taifa hili linatutegemea sisi ndiyo tunaoumba taifa, tukizalisha wahitimu wasiokuwa na maadili mema, tutambue kuna wakati kwenye maisha ya Taifa letu tutakua na viongozi wasiokuwa na maadili mema na kwa msingi huo taifa letu litapata matatizo makubwa tena pengine kipindi ambacho hatutakuwepo ama tutakua tumezeeka sana hivyo watoto ama wajukuuzetu watakua wahanga wa makosa tunayoyafanya leo.

Tunaposherehekea tujitathimini je ni alama gani tutaacha kwa wanafunzi wetu? Tujiulize je tutakumbukwa kwa jambo gani hata baada ya kustaafu? Je wanafunzi tunaofundisha wanafurahia uwepo wetu madarasani? Na, je? Wanaelewa kwa kiwango cha juu yale tunayofundisha?

Walimu wenzangu nawaomba sana tushirikiane kwa kila namna kumwondoa adui yetu mkubwa ujinga, maradhi na magonjwa. Bahati njema maadui wote hawa huondolewa kwa urahisi na Elimu ambayo sisi ndo tunaoitoa kwa watoto wa Taifa letu.

Tuendelee bila kuchoka kukumbushana wajibu wetu na tuufanye wajibu huo kwa nguvu zetu zote,ili tutakapokua tukidai haki zetu kusiwe na lawama yoyote kwetu. Wala tusiangaliane kwa madaraja ya elimu zetu.

Natoa wito kwa jamii ya kitanzania, ikumbuke kuwa mtu anaekaa kwa muda mrefu na mtoto wako ni mwalimu. Maisha ya mtoto yanajengwa na mwalimu kwa kiasi kikubwa. Ni muhimu na ni lazima ikiwa tunawapenda watoto wetu na Taifa letu basi tuwapende na kuwathamini walimu wetu. Nimezisikia sauti za walimu zikipazwa juu ya kutokuthaminiwa na Mimi kwa macho yangu jinsi baadhi ya jamii zinavyopuuza walimu, nimeona zaidi ya mara mbili wazazi wakiwapiga walimu tena hadharani eti kwa sababu hawakuhudhuria shughuli fulani ya kijamii, nimeona mara kadhaa wazazi wakienda shuleni kupiga wa walimu eti kwa sababu watoto wao wameadhibiwa.
Matukio Kama haya huwavunja moyo sana walimu.

Tunaposherekea siku hii ya leo, niombe serikali iendelee kuwathamini walimu wa Tanzania. Iinue hadhi ya mwalimu kwa kuwaondolea maudhi madogo mdogo mfano kuwalipa madei yao, kujiepusha na utoaji wa kauli ambazo zinaweza kujenga dhana kwa jamii kwamba kazi hii ni ya kawaida mno.

Mwalimu day, ama siku ya mwalimu duniani impe nafasi kila mmoja wetu kutafakari anamthamini vipi mwalimu. Tujikumbushe je ni mara ngapi tumeawatia moyo walimu wetu katika kazi yao? Tujiulize hivi ni kweli tunaweza kusahau kwa haraka namna hii juu ya mchango wa mwalimu kwenye maisha yetu? Ikiwa hatuwezi kuusahau mchango wa mwalimukwenye maisha yetu, basi tutambue tuna deni kubwa kwa walimu wetu, na deni lenyewe ni kuinua hadhi ya mwalimu.

Binafsi najitakia na kuwatakia walimu wenzangu siku njema ya mwalimu duniani.

Mwl Doto Biteko(mb)
Jimbo la Bukombe.

Comments