Mshitakiwa Mauaji ya Mwangosi Ana Kesi ya Kujibu



Mahakama Kuu Kanda ya Iringa imetupilia mbali ombi la kumuachia huru mtuhumiwa wa mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha Channel 10 mkoani humo, Daudi mwangosi na badala yake imesema ana kesi ya kujibu.

Akitoa uamuzi wa ombi hilo mahakamani hapo jana, Jaji Paulo Kihwelo, alisema mahakama imeona mtuhumiwa huyo ana kesi ya kujibu na anatakiwa  kupeleka mashahidi makamanani.
  
Akizungumzia uamuzi huo, wakili wa upande wa utetezi, Rwezaura Kaijage, alisema wameridhika na watatoa ushahidi wakiwa na shahidi mmoja ambaye ni mtuhumiwa mwenyewe.
  
“Utetezi tumeridhika na uamuzi wa mahakama, shahidi atakuwa mmoja na ni mtuhumiwa mwenyewe, lakini tunaiomba mahakama yako tukufu ushahidi huo utolewe kwa njia ya kiapo,” alisema.
  
Kaijage aliomba utetezi huo utolewe leo kuanzia saa 3: 00 asubuhi. Kwa upande wa wakili wa Jamhuri, Ladislaus Komanya na mwenzake Sunday Hyera, walisema hawana pingamizi lolote la ombi hilo kuwa utetezi utolewe leo.
  
Ulinzi Mkali Mahakamani
Kabla ya Jaji kuingia kwenye chumba cha mahakama, ulinzi mkali wa polisi ulitawala nje na ndani ya mahakama, wakiwamo askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kuzingira eneo hilo.
  
Aidha, waandishi wa habari walipata wakati mgumu kutekeleza kazi yao baada kunyimwa kuingia ndani ya chumba cha mahakama kwa kisingizio kuwa kesi haijaanza, hali iliyolazimu Msajili wa Mahakama hiyo, Ruth Massam, kuingilia kati na kuwataka polisi kuacha lakini hawakumsikiliza.
  
Baada ya mvutano huo, waandishi walikaguliwa na kisha kuruhusiwa kuingia, lakini hali iliendelea kuwa ngumu ndani ya chumba cha mahakama kiasi cha kutishiwa kuvunjiwa vitendea kazi vyao na baadhi ya polisi.
  
Hata hivyo, waaandishi waliendelea kutekeleza majukumu yao hadi kesi ilipoanza.
  
Baada ya Jaji Kihwelo kuahirisha kesi hiyo, mtuhumiwa alishuka kizimbani kimgongo mgongo ili asionekane sura, huku askari wenzake wakimfunika kwa kitambaa na kitenge kichwani, pamoja na bahasha ya kaki. Askari zaidi ya 30 walimzingira ili asipigwe picha.
  
Mwangosi aliuawa Septemba 2, 2012 kwenye ufunguzi wa matawi ya Chadema katika kijiji cha Nyololo, wilayani Mufindi, mkoani Iringa.

Comments