Waziri Mkuu: Wanafunzi Wote Nchini Watakalia Madawati


Serikali imewahakikishia Watanzania kuwa inaendelea kuweka utaratibu kuongeza madawati na miundombinu ya vyumba vya madarasa nchini, kuhakikisha wanafunzi wote wanaokaa chini na kurundikana madarasani, wanapata madawati na vyumba vya kutosha.

Lakini, imesema hawawazuii wadau mbalimbali ikiwamo watanzania, kuchangia katika kuongeza miundombinu hiyo huku wabunge wakipongezwa kwa kuunga mkono serikali kwa kuchangia madawati.

Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa alisema hayo bungeni jana wakati akijibu maswali ya papo na hapo na kueleza kuwa ni jukumu la serikali kumaliza mirundikano hiyo na watafanyia kazi.

Waziri Mkuu alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Ester Mahawe (CCM) aliyetaka kujua baadhi ya wananchi wanaodaiwa kulipa kodi mara mbili na kutofaidika na sera ya elimu bure.

Akijibu swali hilo, Majaliwa alisema suala la elimu bure limekuwa likichanganywa na wakati mwingine kupotoshwa.

Alisema elimu bure ni mkakati unaolenga katika elimu ya msingi na sekondari kwa lengo la kuwapunguzia mzigo wazazi kwa kupunguza michango iliyokuwa inawakwaza .

Alisema wameanza na maeneo ambayo wameondoa ada kwa sekondari Sh 20,000 hadi 70,000, ulinzi, maji umeme na mitihani kwa kutenga fungu kuipa shule kulipia ili wazazi wasipate mzigo wa michango na wanaendelea kuangalia maeneo mengine wanayochangia ili kuwapunguzia mzigo.

Comments