TAARIFA YA KAMATI YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI 20 May, 2016




Jengo la Bunge






JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
BUNGE LA TANZANIA
­­­­­­­­­­­________________






TAARIFA YA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI KUHUSU UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI KWA MWAKA WA FEDHA 2015/2016 PAMOJA NA MAONI YA KAMATI KUHUSU
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA
 WA FEDHA 2016/2017
_______________






MEI, 2016




TAARIFA YA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI KUHUSU UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI KWA MWAKA WA FEDHA 2015/2016 PAMOJA NA MAONI YA KAMATIKUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA
 MWAKA WA FEDHA 2016/2017
________________________
                                                                                         

1.0                 UTANGULIZI


Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 99 (9) na Kanuni ya 117(11), ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Januari, 2016, naomba kuwasilisha Taarifa ya Kamati ya kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Nishati na Madini kwa Mwaka wa Fedha   2015/2016, pamoja na Maoni ya Kamati kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016 /2017.

Mheshimiwa Spika, Kamati ilikutana kwa lengo la  kupokea na kuchambua Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016 na kupitia Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Mheshimiwa Spika, Katika kufanikisha jukumu hili, Kamati ili tekeleza shughuli zifuatazo:-
i)       Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo iliyoidhinishiwa Fedha kwa mujibu wa Kanuni ya 98(1) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Januari, 2016.
ii)     Mapitio ya Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2015/2016 kwa mujibu wa Kanuni ya 98(2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge.
iii)   Uchambuzi wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hii kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Mheshimiwa Spika, Taarifa hii inaonesha matokeo ya shughuli hizo pamoja na Maoni na Ushauri wa Kamati kwa mujibu wa Kanuni ya 99(9) ya Kanuni za Kudumu za Bunge.

2.0         UKAGUZI WA MIRADI YA MAENDELEO ILIYOTENGEWA FEDHA KWA MWAKA 2015/2016


Mheshimiwa Spika, Kamati ilizingatia masharti ya Kanuni ya 98(1) ya Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Januari, 2016 kwa kutembelea  Mikoa ya Dar Es salaam, Mtwara, Manyara, Njombe na Mbeya kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo chini ya Wizara ya Nishati na Madini iliyotengewa na kupelekewa Fedha kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016. Naomba kulijulisha Bunge lako Tukufu kuhusu miradi hiyo kama ifuatavyo:-
i)       Kinyerezi I MW 150.
ii)     Bomba la Gesi Mtwara
iii)    Mgodi wa Tanzanite one,
iv) Makambako/Songea Transimission Line wenye  msongo wa  kilovoti   220
v)   REA katika  vijiji vya mkoa wa Njombe pamoja na
vi) Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira.

2.1                                 Maelezo kuhusu Miradi ya Maendeleo iliyokaguliwa
Mheshimiwa Spika, Miradi iliyokaguliwa na Kamati kwa ujumla wake inahusu mambo muhimu yafuatayo;
i)                   Uzalishaji wa Umeme wa Kinyerezi I MW 150;

ii)                 Bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam pamoja na mitambo ya kuchakata na kusafisha gesi ya Mnazi bay na Songo Songo;

iii)               Mradi wa Makambako/Songea wa   kusambaza umeme katika mikoa ya Ruvuma na Njombe. Kamati ilikagua utekelezaji wa mradi katika vijiji vya Lyamkena, Itipingi, Igongolo na Tagamenda;

iv)             Mradi wa REA katika Mkoa wa Njombe. Kamati ilikagua utekelezaji wa mradi huo katika vijiji vya Itulahumba, Isindangosi, Iteni, Usuka, Mlevela pamoja na Nyumbanitu na Kichiwa;

  
v)               Mgodi wa Tanzanite One;
vi)              Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira;
                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                               
2.2       Matokeo ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016

2.2.1                          Miradi ya Sekta ya Nishati

2.2.1.1                                         Mradi wa REA
Mheshimiwa Spika, Miradi ya REA  inagharamiwa na fedha za Mfuko wa Nishati Vijijini ambao vyanzo vyake vya Mapato ni pamoja na  tozo ya shilingi 100 katika kila lita ya mafuta ya Petroli na Dizeli na shilingi 150 katika kila lita ya  mafuta ya taa.  Kamati inasikitishwa na hali ya kusua sua katika  upelekaji wa fedha za miradi ya REA, licha ya fedha hizo kuwekewa wigo wa kisheria( Ring fenced).

Takwimu zinaonesha kwamba tangu Tozo hizi ilipoanza kukusanywa Julai 2013 hadi kufikia Machi, 2016 jumla ya shilingi Bilioni 493.8 zimekusanywa kutoka kwenye tozo za Petroli na Dizeli, shilingi bilioni 448.5 kutoka kwenye Mafuta ya Taa na shilingi bilioni 45.4 kutoka kwenye Custom Processing Fee.
Mheshimiwa Spika, licha ya makusanyo hayo, kiasi cha fedha kilichopelekwa kwenye Mfuko wa Nishati Vijijini hadi Aprili 2016 ni shilingi bilioni 366.95 s.awa na asilimia 37.15 ya makusanyo yote kutoka kwenye Tozo hizo.

Aidha, Kamati hairidhishwi na mwenendo wa utolewaji wa fedha za bajeti zinazoidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi ya REA.  Takwimu zinaonesha kwamba, katika miaka mitatu ya fedha iliyopita (2013/14 hadi Aprili 2015/16 wastani wa upatikanaji wa fedha za REA ulikuwa ni kwa asilimia 60. Ufafanuzi kuhusu mwenendo wa upatikanaji wa fedha kwa kipindi cha miaka mitatu umeelezwa katika jendwali lifuatalo:-
Mwaka wa Fedha
Fedha iliyoidhinishwa
Fedha iliyotolewa
Asilimia ya Lengo
2013/2014
Bilioni 285.5
BIlioni 184.9
65
2014/2015
Bilioni 271.6
Bilioni 189.7
70
2015/2016
Bilioni 357.1
Bilioni 168.9
Hadi Aprili 2016
47.3

Mheshimiwa Spika, Kamati  inahoji  juu ya  wapi zilipo shilingi bilioni 73.5 ambazo ni tofauti ya tozo zilizokusanywa na Mfuko wa Nishati Vijijini katika kipindi cha miaka mitatu ikilinganishwa na bajeti iliyoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya REA? Kutojulikana zilipo fedha hizo kuna leta hisia kwa Kamati kwamba fedha hizi zina matumizi mengine tofauti na yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, Kamati inalishauri Bunge lako liitake Serikali itoe ufafanuzi wa kina ni kwanini fedha hizi ambazo ukusanyaji wake ni wa uhakika na zimewekewa wigo kisheria (Ring fenced) hazipelekwi kwenye utekelezaji wa miradi REA? Vinginevyo Kamati haioni mantiki ya kuweka tozo kwenye mafuta nakuendelea kumuumiza wanachi ilihali fedha hizo hazitekelezi jambo lilokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, kutotolewa kwa fedha za REA kikamilifu kumekuwa na athari mbalimbali katika usambazaji wa umeme vijijini, ikiwa ni pamoja na Wakandarasi wanaotekeleza miradi ya REA kutolipwa kwa wakati jambo linaloongeza gharama za mradi. Aidha, utaratibu unaidhihirishia Kamati kuwa, Wizara haitaweza kufikia malengo ya kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa Sekta ya Nishati kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni TANESCO kushindwa kushindwa kusimamia kikamilifu Wakandarasi wanao  tekeleza miradi na hivyo kusababisha miradi hiyo kutekelezwa chini ya kiwango.   Kwa mfano katika mkoa wa Njombe Wakandarasi walifunga mashine Humba (Transformers) 60 zilizochini ya kiwango hadi wakati Kamati inafanya ziara mashine 35 kati ya hizo zilikuwa zimeisharibika.

2.2.1.2      Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira
Mheshimiwa Spika, iwapo Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira utaanza uzalishaji, utaongeza umeme kwa MW400. Uzalishaji huu utaboresha upatikanaji wa umeme na kuchangia kufikiwa  kwa azma ya nchi yetu kuingia katika uchumi wa Viwanda. Hata hivyo, kamati inasikitishwa kuwa haioni dhamira ya dhati ya Serikali kuendeleza Mgodi huu kutokana na sababu zifuatazo:-

Moja, kiasi cha fedha ambacho kimekuwa kikitengwa kwa ajili ya mgodi huu ni kidogo sana na kisicho zingatia mahitaji ya Mgodi, Kwa mfano kiasi cha fedha kinachohitajika ili mgodi uweze kuanza uzalishaji wa MW 50 kwa awamu ya kwanza unahitaji jumla ya shilingi bilioni 145 lakini katika mwaka wa fedha  2015/2016  mgodi uliidhinishiwa shilingi Bilioni  2 tu.  Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017 mgodi umetengewa kiasi kile kile.

Mbili, kutopelekwa kwa fedha zinazoidhinishwa. Kamati imebaini kwamba, licha ya fedha zinazoidhinishwa kwa ajili ya mgodi kuwa ni kidogo fedha hizo hazipelekwi. Kati ya shilingi bilioni 2 zilizoidhinishwa katika mwaka wa fedha 2015/2016 hakuna fedha yoyote iliyopelekwa hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Aprili 2016.

Tatu, Serikali kutokuwa na mkakati wa kupata matumizi mengine ya madini haya, kunalipunguzia Taifa pato kubwa ambalo lingeweza kupatikana kupitia Makaa ya mawe. Kamati inaishauri Serikali kufanya mazungumzo na Viwanda vya simenti ili vitumie makaa ya Mawe yanayozalishwa hapa nchini. Mfano:- Kiwanda cha DANGOTE kinatumia Makaa ya Mawe kutoka Afrika Kusini.

Mheshimiwa Spika, Kamati inashauri Serikali kuwa kama haijawa na dhamira ya dhati ya kuanzisha uzalishaji katika Mgodi huu ni vema Bajeti kidogo inayotengwa ikaelekezwa katika Miradi mingine ya Nishati.

2.2.1.3     Mradi wa njia ya kusafirishia umeme wa msongo wa kilovoti 220 wa Makambako/Songea 
Mheshimiwa Spika,  Mradi huu  unaotekelezwa kwa ufadhili kwa pamoja baina ya Serikali ya Swedeni na Tanzania, unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovolti 220 yenye urefu wa kilometa 250 kutoka Makambako hadi Songea, ambayo inatarajiwa kuwa na uwezo wa kusafirisha (carrying capacity) MW 150 za nishati ya umeme. Aidha, mradi huu muhimu kwa mikoa ya Njombe na Ruvuma  umeshindwa kukamilika kwa wakati kutokana changamoto ya upatikanaji wa fedha za kulipa Wakandarasi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, hatua ya Kamati yako kufanya ziara ya ukaguzi  imesaidia  mradi huo kupelekewa fedha zilizokuwa zimekwamba kutoka Hazina. Hali hii inadhihirisha kwamba fedha ya mradi ilikuwepo lakini hakuwa na dhamira ya kuipeleka.

Utaratibu huu wa kuchelewesha fedha za miradi umekuwa ukiingizia Serikali hasara kwani imekuwa ikilazimika kulipa fidia kwa Wakandarasi kutokana na kuchelewesha malipo.

2.2.2                Miradi Sekta ya Madini
2.2.2.1     Madini ya Vito
2.2.2.1.1       Madini ya Tanzanite
Mheshimiwa Spika, Tanzanite ni madini yanayopatikana Tanzania peke yake, hata hivyo kama Taifa tumekuwa hatunufaiki na mapato yanayotokana na uchimbaji wake, kutokana na Serikali kukosa mfumo madhubuti wa usimamizi. 

Vilevile, kukosekana   kwa miundombinu ya kukata Tanzanite hapa nchini kumesababisha Wawekezaji pamoja na wachimbaji wadogo wadogo kutorosha madini nje ya nchi kwa kigezo cha kwenda kuyasafisha.  Jambo hili siyo tu kwamba lina ikosesha nchi mapato stahiki, bali linatufedhehesha kama Taifa pekee linalozalisha madini haya dunia   kwa kutufanya tushike nafasi ya nne nyuma ya nchi za India, Afrika Kusini na Kenya katika uuzaji wa Tanzanite.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hakuna dhamira ya dhati ya Serikali ya kudhibiti utoroshaji wa Tanzanite ghafi, kamati inashauri kuwa  usimamizi wa Mgodi huu uangaliwe upya ili kulinda  rasilimali hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, Kamati inasikitishwa na jitihada finyu za kutafutia ufumbuzi wa mgogoro wa muda mrefu kati ya Wachimbaji wadogo na mwekezaji. Mgogoro huu unatokana na muingiliano wa maeneo ya uchimbaji chini ya ardhi (maarufu kama “mitobozano”). Pia Sheria ya madini inachangia ukuaji wa mgogoro huu kwa kukosa vifungu vinavyoelezea uchimbaji wa madini ya Tanzanite, ambao ni tofauti ikilinganishwa na uchimbaji wa madini mengine.

Serikali   imeunda   Tume zaidi ya 6 kati ya mwaka 2002 hadi 2008  kwa lengo la kutafuta ufumbuzi wa mgogoro baina ya Wawekezaji na Wachimbaji wadogo wadogo. Hata hivyo, Maoni na ushauri wa Tume hizi haujafanyiwa kazi jambo linalisababisha kuendelea kukua kwa mgogoro huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa juhudi za Serikali katika kushughulikia mgogoro huu zimeonekana kushindwa, Kamati inalishauri Bunge lako tukufu lifuatilie kwa kina mgogoro huu kwa maslahi ya Taifa letu.

2.2.2.1.2       Madini ya Almasi
Mheshimiwa Spika, pamoja na uchimbaji wa muda mrefu wa Almasi hapa nchini, Taifa limekuwa halinufaiki na mapato yatokanayo na rasilimali hii. Mgodi pekee unaochimba madini hayo wa Mwadui umekuwa haulipi Corporate Tax kama inavyotakiwa kisheria kwa kisingizio cha kuzalisha kwa hasara.

Kwa mujibu wa takwimu za Mamlaka ya Mapato Tanzania, mgodi huu umelipa kodi ya mapato (corporate tax) kwa miaka minne tu ambayo ni kuanzia mwaka 2008/2009 hadi 2013/2014.

Mheshimiwa Spika, Kamati haiamini kwamba mgodi huu umekuwa ukijiendesha kwa hasara kwa miaka yote ambayo umekuwa ukifanya shughuli za uchimbaji wa madini hayo kama unavyodai. Iwapo madai hayo yangekuwa na ukweli wowote, ni wazi kwamba mgodi ungekuwa umeshafunga  shughuli za uzalishaji.

2.2.2.2     Madini ya Dhahabu

Mheshimiwa Spika, uchambuzi wa Kamati umebaini kuwa migodi mikubwa ya dhahabu nchini hailipi kodi ya mapato (Corporate tax) kwa kisingizio cha kupata hasara endelevu katika uzalishaji.  Hata hivyo kamati haikubaliani na sababu hiyo kwani taarifa zinaonesha kwamba makapuni yanayomiliki migodi hiyo yamekuwa yakipata faida kwenye masoko ya hisa ambako kampuni hizi zimesajiliwa.

Aidha, Ripoti ya TMAA ya mwaka 2015 inaonesha kwamba makapuni ya madini ya dhahabu hayakulipa jumla ya shilingi bilioni 10.27 kwaajili ya ushuru wa Huduma (Service Levy), na Mrabaha (Royalty) kwenye Halmashauri husika. Kamati inaitaka  Serikali  ifuatilie  malipo ya tozo hizo.

Mheshimiwa Spika,  Kamati  inasikitishwa na  ulipaji mbovu wa kodi  kwa mgodi wa ACACIA (zamani Baarick gold na African Barrick Gold) kwa kutolipa kodi ya zuio         (Withholding Tax) na kodi ya mapato(Corporate Tax) kwa miaka minne hata baada ya kuamriwa na mahakama ya usuluhishi  kulipa kodi hiyo inayofikia jumla ya  shilingi bilioni 89.

Kamati inaitaka Serikali kuchukua hatua  madhubutu  juu ya mwenendo huo. Ili iweze kudhibiti ukosefu wa mapato kama ilivyotokea kwenye migodi ya Resoulte na Tulawaka ambayo ilifunga shughuli za uchimbaji bila kulipa kodi stahiki.

Mheshimiwa Spika, kamati inatambua jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Serikali katika kuwawezesha Wachimbaji wadogo wadogo katika shughuli zao za uchimbaji kwa kuwatengea maeneo ya uchimbaji, kuwapa ruzuku na kuwajengea uwezo kupita mafunzo mabalimbali. Hata hivyo, jitihada hizi bado hazijakidhi mahitaji kwani kumekuwa na malalamiko ya Wachimbaji wadogo wadogo kukosa maeneo ya uchambaji pamoja na mitaji.

Pia Wananchi wa maeneo yanayozunguka migodi waliochukuliwa maeneo yao wamekuwa wakilalamika juu ya kucheleweshewa au kutolipwa fidia zao.  Mfano mzuri ni wananchi wa maeneo ya Nyamongo na Nyamichele yanayozunguka mgodi wa North Mara ambao maeneo yamechukuliwa na Mgodi zaidi ya miaka mitatu iliyopita lakini hawajalipwa faidi hali hii inawafanya wananchi hawa kuishi maisha ya shida na kushindwa kuendeleze shughuli zao mbalimbali.

2.3           Miradi ya Gesi.
Mheshimiwa Spika, Sekta ya gesi asilia ina fursa kubwa ya kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Hata hivyo ugunduzi wa rasilimali hiyo umeendelea   kubainika katika nchi mbalimbali zikiwemo nchi jirani.  Masoko tunayotegemea kuuza gesi yetu ndiyo ambayo yana tegemewa pia na nchi nyingine zenye gesi.

Katika mazingira ya aina hii ni wazi kwamba tutegemee ushindani mkubwa wa biashara ya gesi kwa kuzingatia nguvu ya soko ambayo zinaonesha kwamba kuna uwezekaano uzalishaji wa gesi ukawa mkubwa kuliko mahitaji (global oversupply of gas against low demand). 

Mheshimiwa Spika, Hata hivyo, malengo ya Serikali ya kuanza kuuza gesi nje ya nchi ifikapo mwaka 2023 yanaweza yasifikiwe kutokana na kasi ndogo ya Serikali katika kukamilisha ujenzi wa mtambo wa kusindika gesi asilia (LNG plant). Sambamba na hilo kuwe na mkakati madhubuti kuhusu matumizi ya ndani ya gesi asilia kwa lengo la kutumia kikamilifu soko la ndani kabla ya kuatafuta soko la nje.
Hata hivyo,  kamati inaipongeza Serikali kwa kuanza kutumia soko la ndani kwa kuwezesha gesi hiyo kutumika katika mitambo ya Kinyerezi I ambayo inauwezo wa kuzalisha MW 150.
2.4       Maoni ya Jumla kuhusu Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo kwa mwaka wa fedha 2015/2016
Mheshimiwa Spika, kutokana na ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo Kamati  inatoa  maoni yafuatayo:-

i)                   Serikali iandae Mpango mkakati utakaowezesha usimamizi na matumizi wa Gesi asilia. Kamati inashangazwa na Kiwanda cha Dangote kutotumia Gesi inayozalishwa Mtwara.
ii)                 Serikali iharakishe ukamilishwaji wa Mradi wa usindikaji gesi (Liquefied Natuaral Gas) utakaowezesha gesi hiyo kusafirishwa kwa urahisi.
iii)               Kuwe na usimamizi mzuri na wa karibu kwa Wakandarasi wanao tekeleza miradi ya maendeleo hususan Miradi ya REA.
iv)             Serikali itenge fedha za kutosha na kuzipeleka kwa wakati kwenye miradi ya kimkakati kama vile Mgodi wa makaa ya Mawe wa Kiwira.

v)               Serikali iwekeze katika miundombinu na utaalamu wa madini ya vito ili kuwezesha ukataji na uuzaji wa Tanzanite kufanyika hapa nchini.

vi)             Madeni ya Wakandarasi  yalipwe kwa wakati ili kuepusha ongezeko la  gharama linalotokana na Serikali kulipa fidia.

vii)           Serikali itatafute namna bora ya kumaliza migogoro ya mrefu ya baina ya Wawekezaji na Wachimbaji wado wadogo.

3.0       UCHAMBUZI WA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA BAJETI NA UZINGATIAJAI WA MAONI YA KAMATI  KWA MWAKA WA FEDHA WA 2015/2016

Mheshimiwa Spika, Kamati ilifanya  uchambuzi wa  Bajeti kwa kuzingatia mambo makuu matatu ambayo ni Makusanyo ya Maduhuli kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Hali ya upatikanaji wa fedha kutoka Hazina na Uzingatiaji wa maoni na ushauri uliotolewa na Kamati ya Nishati na Madini wakati huo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliarifu Bunge lako tukufu kuhusu matokeo ya uchambuzi huo kama ifuatavyo:-

3.1       Uchambuzi wa Taarifa kuhusu Ukusanyaji wa Maduhuli kwa mwaka wa fedha 2015/2016


Mheshimiwa Spika, Wizara ilipanga kukusanya maduhuli jumla ya Shilingi bilioni 291.98 sawa na asilimia 45.5 ya bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2015/2016. Taarifa ya utekelezaji inaonesha kuwa, hadi kufikia Machi, 2016, Wizara ilikuwa imekusanya jumla ya shilingi bilioni 157.64 sawa na asilimia 54.99 ya lengo.

Mwenendo huu ni ishara ya kutofanikiwa kwa lengo la makusanyo ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016.  Ni Maoni ya Kamati kwamba, Wizara iweke makadirio ya makusanyo ambayo ni halisi badala ya kuwa na makadirio makubwa yasiyotekelezeka.

Mheshimiwa Spika, Kamati imebaini kuwa mchango wa idara ya Madini kwa mwaka fedha 2016/2017 umeshuka kwa asilimia 19.4 ikilinganishwa na Mwaka 2015/16  wakati mchango wa idara ya  Nishati umeongezeka kwa asilimia 25.5 ikilinganishwa na Mwaka 2015/16.

Ufafanuzi zaidi  umeoneshwa kupitia Jedwali Na. 01 la  Taarifa hii.




2015/2016
2016/2017
VYANZO VYA MAPATO
KIASI
ASILIMIA
KIASI
ASILIMIA
IDARA YA MADINI
211,962,385,000
72.6
215,962,385,000
58.3
IDARA YA NISHATI
79,697,501,000
27.3
154,377,501,000
41.6
IDARA NA VITENGO VINGINE
324,000,000
0.1
344,003,000
0.1
JUMLA KUU
291,983,889,000
100
370,683,889,000
100

Aidha Kamati ilielezwa sababu zilizosababisha kushuka kwa makusanyo kwa Mwaka wa Fdha 2015/2016 kama ifuatavyo:-
i)       Kushuka kwa bei ya dhahabu katika Soko la Dunia
ii)     Kupungua kwa uzalishaji katika Migodi; na
iii)   Kupungua kwa shughuli za utafiti katika Sekta za Nishati na Madini;


3.2       Upatikanaji wa Fedha kutoka Hazina

Katika Mwaka wa Fedha 2015/2016 Wizara ya Nishati na Madini iliidhinishiwa jumla ya shilingi bilioni 642.12 kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake. Taarifa ya Wizara inaonesha kuwa, Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 20151/2016 imeongezeka hadi kufikia  shilingi bilioni 762.12 sawa na asilimia 18 ya bajeti iliyoidhinishwa na Bunge. Ongezeko hili limetokana na uhamisho wa fedha za ndani  wa shilingi bilioni 120 ili kuongeza bajeti ya utekelezaji wa Mradi wa KInyerezi II MW 240 na ulipaji wa sehemu ya madeni ya Ankara za umeme yanayodaiwa na TANESCO na Taasisi za Serikali.

Mheshimiwa Spika, Kamati inapongeza jitihada za Serikali kwa nia yake ya dhati ya kuanza  kutekeleza Mradi huu Muhimu ambao utaweza kuzalisha umeme wa  MW 240,  ongezeko hili la MW 240 katika Grid ya Taifa itasaidia kupunguza tatizo la upatikanaji wa umeme katika maeneo mbali mbali ya nchi hii  na kuwaletea wananchi maendeleo yanayokusudiwa hasa maendeleo ya Viwanda.

Mheshimiwa Spika, Hadi kufikia mwezi Machi, 2016 Wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi bilioni 625.34 sawa na asilimia themanini na mbili 82.  Kati ya fedha  hizo   shilingi bilioni 579.54  zilikuwa ni fedha za Miradi ya Maendeleo sawa na asilimia tisini na tatu 93 ya fedha zilizopatikana hadi kufikia Machi, 2016.  Katika fedha hizo shilingi bilioni 546.18 sawa na asilimia  tisini na nne nukta mbili  94.2 ni fedha za ndani na shilingi bilioni 33.36 sawa na asilimia tano nukta nane   5.8 ni fedha za nje.


Mheshimiwa Spika, ili kutoa picha halisi ya uwiano kati ya Bajeti iliyoidhinishwa na fedha zilizopatikana.

Jedwali Na. 2 la tarifa hii linafafanua
BAJETI ILIYOIDHINISHWA 2015/2016
FEDHA ILIYOPATIKANA HADI MACHI,2016
UFAFANUZI
KIASI
ASILIMIA
KIASI
ASILIMIA
JUMLA KUU
642.12
100
625.34
97.4
FEDHA ZA MAENDELEO
502.3
78.2
579.54
115.4
MATUMIZI YA KAWAIDA
139.82
21.7
45.8
33
CHANZO: Taarifa ya Wizara ya Nishati na Madini  fungu 58 kuhusu utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2015/2016.

Mheshimiwa Spika,  Kamati imefanya upembuzi yakinifu wa hali ya upatikanaji wa fedha unaonesha kuwa Wizara ilipata fedha za kugharamia miradi ya maendeleo kwa kiasi kinachozidi Bajeti  iliyoidhinishwa na Bunge lako tukufu kwa mwaka wa fedha 2015/2016,  kama inavyofafanuliwa  katika Jedwali namba mbili la tarifa hii.

Mheshiiwa Spika, Kutokana na ongezeko hilo, Kamati ilitaka kupata maelezo ya kina ili kulinganisha upatikanaji wa fedha na bajeti  iliyoidhinishwa.
  Aidha, ni maoni ya kamati kuwa  ili kuwe na utekelezaji bora wa Bajeti, Wizara inapaswa kuzingatia mahitaji halisi, vipaumbele na uwezekano wa upatikanaji wa fedha kwa kufanya hivyo, itakuwa si rahisi  upatikanaji wa fedha kuzidi kiasi cha Bajeti inayoidhinishwa na Bunge.

3.3       Mapitio ya Utekelezaji wa Ushauri wa Kamati

Mheshimiwa Spika, wakati wa kuchambua Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016, Kamati ilitoa Maoni, Ushauri na Mapendekezo katika maeneo ya Umeme, Gesi asilia, Biashara ya Mafuta, Utendaji wa Wizara na Taasisi chini ya Wizara. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa baadhi ya Ushauri uliotolewa na Kamati haukuzingatiwa na kufanyiwa kazi na Serikali kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, bado kuna tatizo la kukaimisha Watendaji Wasaidizi kwa muda mrefu bila kuwapatia mamlaka kamili ya kiutendaji. Tatizo hili lipo STAMICO na Chuo cha Madini. Hali hii inaendelea kukwamisha utekelezaji bora wa Mipango ya Maendeleo. Aidha, jitihada za Serikali za kutafutia ufumbuzi suala hili siyo za kuridhisha sana.

Mheshimiwa Spika, Hatua zilizochukuliwa na Serikali kuhusu utekelezaji wa miradi ya  umeme wa jua (Solar Energy),  umeme wa upepo (Wind Energy), umeme wa joto ardhi (Geothermal) na Tungamotaka (Renewable Energy) haioneshi nia ya dhati ya Serikali ya kutekeleza miradi hiyo muhimu hasa kwa kutengewa  bajeti kidogo mwaka 2016/17.


Mheshimiwa Spika, Kamati haikuridhishwa na kasi ya EWURA katika kuwaelimisha na kuwasimamia wajenzi na wamiliki wa vituo vya mafuta hasa katika maeneo ya Vijijini, Kanuni  zilizo andaliwa  kuhusu  Usimamizi wa Ujenzi na Uendeshaji wa Vituo maeneo ya vijijini (The Petroleum (Rural Retail Outlets Operation) Rules, 2015, Kanuni hizi hazifahamiki kwa watumiaji hivyo kuleta usumbufu wakati wa ukaguzi wa vituo kwa kutoza faini ya Shilingi milioni tano hata kama wana vibali vya ujenzi toka Halmashauri na NEMC.

Mheshimiwa Spika, Pamoja na utaratibu mzuri wa fedha za REA uliwekwa kisheria kuhusu fedha zake kulindwa (Ring Fenced) bado upatikanaji wake hauridhishi, Miradi ya REA kwa mwaka uliopita 2015/2016 ulitengewa Shilingi 357.1 na hadi sasa zimepelekwa Shilingi bilioni 168 sawa na asilimia arobaini na saba (47%) ya bajeti yote iliyokuwa imetengwa katika miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kulipa madeni ya TANESCO kupitia Hazina na kwa mwaka 2015/2016 zimelipwa jumla ya Shilingi bilioni 184 ambayo ni sawa na asilimia 59.74 ikiwa ni madeni ya Serikali na Taasisi zake, utaratibu huu wa malipo unakwamisha utekelezaji shughuli mbali mbali za TANESCO.
Aidha, Serikali imeendelea kutekeleza maoni na ushauri wa Kamati kwa kuingiza kwenye Bajeti ya Wizara ya mwaka 2016/17, hivyo utekelezaji unaendelea.

4.0               UCHAMBUZI WA MPANGO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI KWA (FUNGU 58) MWAKA WA FEDHA 2016/2017


4.1     Mapitio ya Malengo ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2016/2017

Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha 2016/2017 wizara imejiwekea Malengo Makuu Matano (5) yafuatayo:-
i)       Kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa Sekta ya Nishati kwa maendeleo endelevu ya Taifa.
ii)     Kuboresha uendelezaji na usimamizi endelevu wa rasilimali za  madini kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi
iii)   Kuimarisha utoaji wa huduma kwa wadau katika Sekta za Nishati na Madini.
iv) Kuboresha utoaji wa huduma kwa watumishi waathirika wa VVU na UKIMWI ili kupunguza maambukizi
v)   Kuondoa vitendo vya Rushwa katika sekta ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Spika, Kamati   ilibaini   kuwa Wizara ya Nishati na Madini imekuwa na malengo haya ya muda mrefu kuanzia mwaka 2011/12 hadi mwaka 2016/17.  Kamati ilitaka kujiridhisha kuhusu kujirudia kwa malengo hayo na kufanya rejea katika Hati Idhini (Government Instrument) iliyochapishwa   katika Gazeti la Serikali Na. 144   la tarehe 22 Aprili, 2016.  Kamati ilibaini kuwa malengo hayo yanaendana na Mpango wa Taifa, aidha Kamati katika uchambuzi wa bajeti imeridhia malengo hayo kutokana na umuhimu wake.

Mheshimiwa Spika, malengo haya yamezingatia majukumu yaliyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Wizara, sura 299, The Ministers (Discharge of the Ministerial Functions) Act.

4.2                             Uchambuzi wa Makadirio ya Mapato
Mheshimiwa Spika, Makisio ya makusanyo ya Maduhuli kwa Mwaka wa Fedha 2016/17 yanakadiriwa kuwa jumla ya Shilingi 370.68 ikilinganishwa na Shilingi bilioni 286.66 kwa mwaka wa fedha 2015/16.  Kati ya makusanyo hayo Shilingi bilioni  215.96 sawa na asilimia 58.3  zitakusanywa na idara ya Madini, shilingi 154.378  sawa na asilimia 41.6 zitakusanywa na idara ya Nishati na shilingi 344,003,000 sawa na asilimia 0.1 zitakusanywa na idara na vitengo vingine katika Wizara.

Makadirio ya makusanyo ya mapato yameongezeka kwa asilimia 29.3 ikilinganishwa na makadirio ya makusanyo ya mwaka 2015/16. Aidha ongezeko hili la Makusanyo ya maduhuli kwa mwaka wa fedha 2016/17 linatokana na sababu zifuatazo:-
i)       Kuendelea kutumia Gesi Asilia badala ya mafuta mazito katika miradi mikubwa ya uzalishaji umeme;

ii)     Kuendelea kuhamasisha shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia ili kuongeza uzalishaji na mauzo;

iii)   Kuendeleza kuimarisha usimamizi wa  wachimbaji wadogo kwa kutoa huduma za ugani na kuwapa mafunzo ili wafuate Sheria katika shughuli zao ikiwa ni pamoja na kulipa Maduhuli ya Serikali;

iv) Wizara kutoa malengo ya ukusanyaji kwa kila Kamishna Msaidizi na Mkazi katika ofisi za Mikaoni;


v)   Kuimarisha ushirikiano na Taasisi nyingine za Serikali katika kuzuia utoroshaji na biashara isiyo rasmi ya madini ikiwa ni pamoja na kuanzisha masoko ya madini ya vito;

vi) Kukuza matumizi ya ndani ya gesi asilia ili kuongeza mapato na kupunguza uharibufu wa mazingira unaotokana na matumizi ya kuni na mkaa.

4.3                               Uchambuzi wa Makadirio ya Matumizi
Mheshimiwa Spika, makadirio ya matumizi ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka 2016/2017 ni jumla ya Shilingi 1,122,845,741,000 ikilinganishwa na Shilingi 642,123,079,000 zilizoidhinishwa na Bunge kwa mwaka 2015/2016, hii ni sawa na ongezeko la asilimia sabini na nne nukta tisa 74.9.  Kamati ilielezwa kuwa ongezeko hili linatokana na kuongezeka kwa fedha za miradi ya Maendeleo.

Aidha, Bajeti ya fedha za ndani za REA imeongezeka kutoka Shilingi 357,117,000,000 mwaka 2015/16 hadi Shilingi 534,400,000,000 kwa mwaka 2016/17, sawa na ongezeko la asilimia arobaini na tisa nukta sita 49.6 ya bajeti ya REA kwa mwaka wa fedha 2015/2016.

Mheshimiwa Spika, Bajeti ya miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2016/2017 inakadiriwa kuwa  jumla ya Shilingi 1,056,354,669,000 ikilinganishwa na Shilingi 502,303,938,000 kwa mwaka 2015/16, ongezeko hilo ni sawa na asilimia mia moja na kumi nukta tatu 110.3. Ongezeko hilo la Bajeti ya Maendeleo ni sawa na asilimia tisini na nne 94 ya Bajeti yote ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, fungu 58  kwa mwaka 2016/2017  fedha za ndani za maendeleo zimeongezeka kutoka shilingi bilioni 280.00 hadi shilingi bilioni 724.84, fedha za nje zimeongezeka kutoka shilingi bilioni 85.35 hadi shilingi bilioni 331.51.

Aidha, bajeti ya matumizi ya kawaida kwa mwaka wa fedha 2016/17 imetengwa jumla ya Shilingi 66,481,072,000 sawa na asilimia sita 6 ya bajeti yote ya Wizara kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 38,654,138,000 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC) na shilingi bilioni  27.83 ni kwa ajili ya mishahara ya Watumishi wa Wizara na Taasisi zake.

Bajeti ya matumizi ya kawaida imepungua kwa kiasi kikubwa sana ukilinganisha na bajeti ya mwaka wa Fedha 2015/16 ambapo ilikuwa shilingi 171,613,498,000 sawa na asilimia thelathini na mbili 32 ya Bajeti yote ya Wizara,  bajeti hii ni pungufu kwa asilimia  38.73 ya bajeti ya mwaka wa fedha 2015/2016.

Mheshimiwa Spika, Bajeti ya Miradi ya Maendeleo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 ni sawa na asilimia 10.04 ya Bajeti Kuu ya Maendeleo ya Taifa.  Bajeti ya Matumizi mengineyo ni sawa na asilimia 0.49 ya Bajeti ya Matumizi ya kawaida ya Taifa, bajeti hii ni pungufu ya bajeti ya mwaka 2015/2016 kwa asilimilia 1.28.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2016/17 bajeti ya  Miradi ya maendeleo imeongeza  kwa asilimaia 110.3 toka kwenye Bajeti ya Miradi ya Maendeleo kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016. Ongezeko hilo litasaidia  kukamilisha miradi kipumbele ya Taifa hasa kwa upande wa Nishati na miradi ya kimkakati kwa Wizara itatekelezwa kwa ufanisi.

5.0               MAONI NA USHAURI WA KAMATI
Mheshimiwa Spika, Kamati katika kutekeleza majukumu yake ya kikanuni ya ukaguzi wa miradi, uchambuzi wa Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa fedha 2015/16 na uchambuzi wa makadirio na matumizi ya Wizara kwa mwaka wa Fedha 2016/17 ufuatao ni ushauri na maoni ya Kamati:- 
i)       Serikali iandae Mpango mkakati utakaowezesha usimamizi mzuri wa Gesi asilia inayozalishwa nchini ikiwa ni pamoja na kutafuta masoko.
ii)     Serikali iharakishe ukamilishwaji wa Mradi wa usindikaji gesi (Liquefied Natuaral Gas) utakaowezesha gesi hiyo kusafirishwa kwa urahisi
iii)      Kuwe na usimamizi mzuri na wa karibu kwa Wakandarasi wanao tekeleza miradi ya maendeleo hususan Miradi ya REA.

iv) Serikali itenge fedha za kutosha na kuzipeleka kwa wakati kwenye miradi ya kimkakati kama vile Mgodi wa makaa ya Mawe wa Kiwira.

v)   Serikali iwekeze katika miundombinu na utaalamu wa madini ya vito ili kuwezesha ukataji na uuzaji wa Tanzanite kufanyika hapa nchini.

vi) Madeni ya Wakandarasi yalipwe kwa wakati ili kuepusha ongezeko la gharama linalotokana na Serikali kulipa fidia.

vii)  Serikali itekeleze kwa dhati ushauri na mapendekezo ya Tume mbalimbali zilizoundwa ili kutua mgogoro wa muda mrefu wa Wachimbaji wadogo wadogo wa Tanzanite.

viii)   Chuo cha Madini kitengewe fedha za kutosha ili kuweza kuzalisha wataalamu watakaoendeleza rasilimali muhimu za Taifa hili.

ix)  Wakandarasi wanaotekeleza miradi mbali mbali walipwe kwa wakati ili kukwepa kulipa fidia zisizo za lazima.

x) Fedha za REA zinazokusanywa kutoka kwenye tozo ziwasilishwe moja kwa moja kwenye Mfuko wa Nishati Vijijini .

xi)  Serikali isimamie  kwa makini ukamilishwaji wa miradi ya vipaumbele ya kuzalisha umeme ili kuwezesha upatikanaji wa umeme wa kutosha na wa uhakika na kwa bei nafuu.

xii)Kamati inaitaka Serikali kuchukua hatua madhubuti na zakupimika katika kusimamia madini haya adimu ya Tazanite ili kuiondoa nchi katika aibu ya utoroshaji wa Madini.

6.0               HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge, kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuliongoza Bunge. Mungu awajalie afya njema, hekima na busara katika kutekeleza wajibu huu mkubwa tuliowakabidhi.

Kwa namna ya pekee nawashukuru Wajumbe wa Kamati kwa ushirikiano walionipa wakati wa kujadili na kuchambua makadirio ya Mapato na Matumizi ya fungu 58 kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Naomba majina yao yaingizwe kwenye Hansard kama yalivyo:-
1.      Mhe. Doto Mashaka Biteko, Mb                  -           Mwenyekiti
2.      Mhe. Deogratius Ngalawa, Mb                   -           M/Mwenyekiti
3.      Mhe. Mohamed Juma Khatib, Mb             -           Mjumbe       
4.      Mhe. Ally Mohamed Keissy, Mb                   -                                
5.      Mhe. Yussuf Kaiza Makame, Mb                 -                               
6.      Mhe. Zainabu Mussa Bakar, Mb                  -                      
7.      Mhe. Haroon Mulla Pirmohamed, Mb      -                      
8.      Mhe. Mwantakaje Haji Juma, Mb              -                      
9.       Mhe. Daimu lddi Mpakate, Mb                  -                      
10.  Mhe. Catherine Valentine Magige, Mb   -                      
11.  Mhe. Oscar Rwegasira Mukasa, Mb         -                      
12.  Mhe. Stella Ikupa Alex, Mb                           -                      
13.    Mhe. Joyce Bitta Sokombi, Mb                   -                      
14.    Mhe. Bahati Ali Abeid, Mb                           -                      
15.    Mhe. Mauled Said Abdalah Mtulia, Mb   -                      
16.    Mhe. Desderius John Mipata, Mb              -                      
17.    Mhe. Katani Ahmad Katani, Mb                 -                      
18.    Mhe. Susan Limbweni Kiwanga,Mb          -                      
19.    Mhe. Vedastus Mathayo Manyinyi, Mb   -                      
20.    Mhe. Bupe Nelson Mwakang’ata, Mb     -                      
21.    Mhe. Maryam Salum Msabaha, Mb         -                      
22.    Mhe. Innocent Lugha Bashungwa,Mb    -                      
23.    Mhe. Ezekiel Magolyo Maige, Mb             -                      
24.    Mhe. Wilfred Muganyizi Lwakatare, Mb   -                      
25.    Mhe. Dunstan Luka Kitandula, Mb             -                      

Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii pia kumshukuru Katibu wa Bunge Dkt. Thomas Didimu Kashilillah, Mkurugenzi wa Idara ya Kamati za Bunge Ndg. Athuman Hussein, Makatibu wa Kamati Ndg. Mwanahamisi Munkunda na Ndg. Felister Mgonja, kwa kuratibu shughuli zote za Kamati na hatimaye kukamilisha Taarifa hii kwa wakati.  Aidha, nawashukuru Watendaji wote wa Ofisi ya Bunge kwa ushirikiano wao ulioiwezesha Kamati kutekeleza majukumu yake kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa Bunge lako Tukufu likubali kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fungu 58 kwa mwaka wa Fedha 2016/2017 ambayo ni Shilingi 1,122,845,741,000.

Mheshimiwa Spika, Naunga mkono hoja na Naomba
kuwasilisha.

Dotto Mashaka Biteko, (Mb)
MWENYEKITI
KAMATI YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI
20 May, 2016                      

Comments

Post a Comment